Katika maisha yetu ya kila siku wapo watu ambaoo haiwezi kupita saa chache bila kuperuzi kwenye mitandao ya kijamii na hii inatokana na utandawazi, teknolojia kwa upana wake lakini hata uraibu pia.
Ni wazi kuwa watu wengi duniani wanaperuzi kwenye Instagram kupitia simu janja nikimaanisha wanaingia kupitia programu tumishi husika lakini wapo wale ambao moja ya tovuti ambazo wanazitembelea kwa kutumia kompyuta ni Instagram. Iwe unatumia programu tumishi/kompyuta nina hakika utakuwa umeshatembelea kipengele cha Insta Stories ambacho kinamuwezesha mhusika kuona machapisho mbalimbali au ya kwake mwenyewe kwa muda usiozidi saa 24.
Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali Instagram wanafanyia majaribio ya muonekano mpya wa Instagram Stories kwenye kompyuta; kwa lugha rahisi kuna maboresho ambayo yamefanyika kwenye kipengele hicho lakini kwa watumiaji wa Instagram kupitia kompyuta za mezani.
Kwa sasa iwapo mtu ataangalia machapisho yaliyowekwa kwenye Stories basi yatachukua ukurasa mzima lakini pia bila ya kuwa na vitufe vya kusogeza ama kurudisha nyuma kuona chapisho kutoka kwa mhusika. Katika maboresho hayo inaaminika kuwa mtumiaji ataweza kuperuzi kipengele hicho kwa urahisi zaidi kupitia kompyuta.
Haijafahamika wazi ni lini maboresho hayo yataanza kupatikana kwa wote baada ya kipindi hiki cha majaribio ambapo ni watu wachache tu ndio ambao wamepewa uwezo wa kuona hayo yaliyoboresha ndani ya kipengele husika ndani ya Instagram kupitia kompyuta.
Vyanzo: Gadgets 360, Engadget
One Comment