Twitter leo imeanza kusambaza toleo jipya la app yake ambalo pamoja na mambo mengine halitahesabia majina ya watumiaji katika idadi ya herufi 140 ambazo mtumiaji anaruhusiwa kutumia katika tweet moja.
Hili jambo sio geni maana liliongelewa saana mwaka jana na mtandao huu uliahidi kuleta mabadiliko haya, baadae walisema mabadiliko haya yangechelewa kuwafikia watumiaji kwa kuwa walikuwa wanawapa washirika muda wa kujiandaa kwa mabadiliko haya.
Katika toleo hilo linaloletwa majina ya watumiaji kama vile @Teknokona na @NdangalasiN hayatahesbika katika ukomo wa herufi 140 kama ilivyokuwa mwanzo, hii inalenga kuwapa uhuru wa kujieleza zaidi watumiaji wa mtandao huu.
Mabadiliko haya kimantiki hayatabadilisha sana namna ambavyo tunaandika tweets zetu hii inatokana na ukweli kwamba sio herufi nyingi ambazo zitaongezeka baada ya mabadiliko haya, kwa wale ambao wanapenda kuandika magazeti msishangilie sana bado safari ya kufika mnakokutaka ni ndefu.
Mabadiliko haya hata hivyo yatawafaa wale ambao huwataja watu wengi katika mazungumzo yao ya twitter kwa maana sasa hivi hawatahitaji kubana maneno yao ili nafasi itoshe.
Ingawa toleo lenye mabadilko haya limeripotiwa kuanza kutoka leo lakini kwa soko la Afrika pengine tunaweza kuhitaji kusubiri kidogo maana ni kawaida kwa mitandao kuachia app kwa baadhi ya masoko kwanza.
Chanzo: Mtandao wa Recode