Ushasikia watu wanasema Facebook pameshakuwa sehemu ya watu wazima na hivyo vijana wadogo wanapaepuka? Inaonekana Facebook pia wameliona hilo na sasa wameleta app ya Lifestage, ambayo ni mtandao wa kijamii kwa vijana wadogo na umebuniwa na kijana mdogo.
Kijana Michael Sayman ambaye amehusika kwa kiasi kikubwa katika utengenezaji wa app hiyo ni mfanyakazi wenye umri mdogo zaidi katika kampuni hiyo anayeshikilia cheo kinachohusika na utengenezaji na usimamiaji (Product Manager) wa app ya Lifestage.
Ukuaji wa apps zingine kama vile Snapchat hasa hasa mafanikio yake ya kuwavutia zaidi vijana hasa hasa wa chini ya umri wa miaka 18 umekuwa tishio kwa Facebook. Tafiti zinaonesha watumiaji wa umri mdogo wa Facebook zaidi ya kufungua akaunti huwa hawapost mambo yao sana tena kwenda mtandao huo kwa kuwa inaonekana wakubwa zao wote wapo humo.
Kwa miaka mingi mfululizo, kuanzia 2014, mtandao wa Facebook umeona idadi ya watumiaji wa chini ya umri wa miaka 17 ikizidi kuporomoka.
Kwa ufupi ni kwamba Facebook inapoteza kwa kiasi kikubwa ushiriki wa vijana wadogo katika mtandao huo. Wapo wanaofungua akaunti na kisha kuachana nazo, wakati huo huo huduma pinzani za Facebook kama vile Snapchat zinazidi kuwa kivutio zaidi hasa hasa kwa vijana.
App ya Lifestage imetengenezwa kwa namna ambayo unaweza ukaifananisha na mtandao wa Facebook miaka ya nyuma wakati umeanzishwa, enzi hizo lazima ujazo shule/chuo unachosoma wakati wa kujiandikisha.
- Ingawa mtu mwenye umri wowote anaweza kufungua akaunti katika app hii ni wale wenye umri wa chini ya miaka 22 ndio wataweza kushiriki kwenye mazungumzo n.k.
- Kama una umri wa juu ya hapo unaweza fungua akaunti tuu ila nje ya hapo mengi hutaweza kufanya
- Kama vile Facebook ilivyoanza zamani, ndani ya Lifestage mahusiano yanajengwa kwa kuangalia shule ambazo wahusika wanasoma
- Na wakishajiunganisha na shule flani basi kuhama tena ni vigumu – huwezi badilisha badilisha
Kwa sasa app ya Lifestage inapatikana kwa watumiaji wa iOS tuu ila inategemewa muda si mrefu itawafikia watumiaji wa Android pia.
Vyanzo: Facebook na mitandao Mbalimbali