Shirika la ujasusi na uchunguzi wa ndani la Marekani la FBI, limewataka watu kuwa makini na Smart TV majumbani kwao. Wadai wadukuzi wanaweza kudukua TV janja kwa urahisi.
Smart TV – ni TV za kisasa zinazokuja na uwezo wa kutumia huduma ya intaneti na hivyo kukuunganisha na huduma mbalimbali za kimtandao kama vile YouTube, Netflix na apps zingine mbalimbali.
Smart TV – Televisheni Janja zipo za aina nyingi kwa sasa, nyingi zikiwa zinakuja na programu endeshaji ya Android.
Shirika la FBI limeweka taarifa ya kuwataka watu kuwa makini na vifaa hivyo huku wakisema vifaa hivyo vinahatarisha usalama wa kidata wa watu.
Kumbuka kwa sasa TV hizi pia zinakuja na kamera na kinasa sauti (microphone).
FBI wamesema “Kuna hatari ya watengenezaji wa TV na apps kuwa wakusikiliza au kukutazama, TV yako inaweza ikawa ni njia ya wadukuzi kuingia nyumbani kwako. Wadukuzi wanaweza lenga kudukua TV yako na kisha kuweza kudukua kifaa chako cha intaneti au vifaa vingine vilivyounganishwa na kifaa hicho kama vile kompyuta”
Wategenezaji TV wamelaumiwa sana ya kwamba hawaweki kipaumbele suala la usalama katika programu endeshaji za TV. Mfano Samsung na LG walishutumiwa mwaka huu ya kwamba TV janja zao zilikuwa zinatuma taarifa kuhusu muvi au tamthilia zinazotazamwa zaidi na wamiliki wa TV zao na kutumia data hizo kwenye matangazo n.k.