Novemba 2 mwaka huu imetimia miaka 20 tokea kituo cha anga cha kimataifa (International Space Station) kianze kutumiwa na wanasayansi wa anga.
Kituo hicho chenye uzito wa zaidi ya tani 420 kinaizunguka dunia mara 16 kila siku kikienda kwa kasi ya zaidi ya kilometa 27,300 kwa saa.
Kituo cha Kimataifa cha anga kinaendeshwa kwa ushirikiano baina ya mataifa mbalimbali hii ikiwa ni pamoja na Marekani kupitia NASA, Urusi kupitia shirika la Roscosmos, Japani, Ulaya kupitia shirika la anga la ESA, pamoja na Kanada kupitia CSA.
Kituo hicho cha anga kinatumika kwa kazi mbalimbali zinazohusu tafiti katika masuala ya anga na afya – jinsi mwili wa binadamu unavyoathirika na kuishi kwa muda mrefu kwenye vyombo vya anga.
Mambo ya kufahamu kuhusu kituo hiki
- Mara zote kituo hicho cha anga kinakuwa umbali wa kati ya kilometa 408 hadi 410 angani, umbali kutoka ardhi ya dunia.
- Ujenzi wake ulianza mwaka 1998, na ulihusisha safari zaidi ya 30 ya vyombo vya anga vya Marekani na Urusi kufanikisha ukalimishaji wake.
- Hadi kukamilika kwake gharama yake ilikuwa zaidi ya dola bilioni 100 (Takribani Trilioni 232 za Tanzania), na kila mwaka kinagharamu zaidi ya dola bilioni 4 (Zaidi ya Trilioni 9 za Kitanzania) kwa ajili ya matengenezo na maboresho.
- asilimia flani ya gharama hii ikihusisha safari za kupeleka wanaanga pamoja na vifaa.
- Wakazi wa kwanza walifika kwenye kituo hicho mwaka 2000 tarehe 2 Novemba, walikuwa wanaanga watatu: Mmarekani Bill Shepherd, Warusi Sergei Krikalev na Yuri Gidzenko.
Tokea kipindi hicho hadi sasa tayari wanaanga tofauti 240 washaishi kwenye kituo hicho kwa nyakati tofauti tofauti.
Kuna wanaoona ya kwamba pesa hizi zinatumika bila faida, na kwamba ni pesa ambazo zingekuwa na mchango mkubwa katika mambo mengine hapa duniani. Ila kuna wanaotetea kwa kusema kituo hicho kina manufaa mengi katika masuala ya kisayansi na tafiti.
Tayari kuna mpango wa kuachia makampuni binafsi kukiendesha katika miaka ijayo, huku serikali zikikodi nafasi pale inapohitajika.
No Comment! Be the first one.