Ijumaa hii (Mei 11) saa 7 mchana Kenya inatarajiwa kurusha satelaiti yake ya kwanza iliyotengenezwa nchini humo na wanafunzi na watafiti wa Chuo Kikuu cha Nairobi kwa ushirikiano na shirika la teknolojia nchini Japan kupitia wakala wake, Japanese Aerospace Exploration Agency (JAXA) pamoja na Chuo Kikuu nchini Italia.
Satelaiti hiyo itarushwa kwenye Sayari kutoka kituo kilichopo Japan, lakini Wakenya kadhaa watapewa nafasi kuhudhuria urushwaji wa Setilaiti hiyo na tukio hilo litakuwa mubashara kupitia kituo cha televisheni cha Kenya cha KBC kuoneshwa kwa Wakenya wote ili kushuhudia tukio hilo kubwa la kihistoria.
Kifaa hicho kuja katika muonekano mpya unaojulikana kama ‘Nano-satellite‘ ambapo inakuwa ni satelaiti ndogo sana katika sura ya mchemraba wa sentimeta 10, na ujazo wa kiasi cha lita moja tu ikiwa na uzito wa kilo 14.
Naibu makamu mkuu wa chuo kikuu cha Nairobi, Profesa Peter Mbithi amesema Setilaiti hiyo imegharimu kiasi cha pesa za Kenya milioni 120 na sehemu kubwa ya pesa hizo zimetolewa na JAXA ambao walitoa $1 milioni.
Maisha ya satelaiti hiyo ni miaka miwili na miezi sita (miezi 30) na baada ya hapo italipuka na kuungua. Pia ndani ya satelaiti hiyo kutakuwa na kamera mbili, kipaza sauti kwa ajili ya kurekodi picha na sauti na kuzituma katika mtandao wake maalum.
Profesa Mbithi amesema kuwa satelaiti hiyo itatumiwa kukusanya data kuhusu masuala mbalimbali muhimu kama mabadiliko ya hali ya anga, uhifadhi wa wanyamapori, utabiri wa hali ya hewa na mambo mengine mengi.
Kenya imeendelea kupata mafanikio ya teknolojia mbalimbali ambazo zinasaidia kuchangia maendeleo ya nchi yao katika kukuza uchumi wa taifa lao.
Vyanzo: Business Daily, Daily Nation