Kampuni ya usalama wa mtandao ya Kaspersky Lab ya Urusi imekiri kuwa iliwahi kupakua kwa bahati mbaya nyaraka za siri za Idara ya usalama ya Marekani (NSA) wakati ilipofanya kazi za kawaida.
Hivi karibuni vyombo vya habari vya Marekani vimeripoti kuwa ushahidi umeonesha kuwa kampuni ya Kaspersky Lab iliwahi kuiba nyaraka kutoka kompyuta ya mfanyakazi wa NSA. Kampuni ya Kaspersky Lab imetoa ripoti ikijibu kuwa baada ya kufanya uchunguzi, imegundua kuwa tukio pekee linalohusiana na habari hii lilitokea mwaka 2014.
Taarifa zinasema wakati huo kampuni hiyo ilikuwa inatafuta kirusi cha “Equation” kwenye mtandao wa intaneti. Mchambuzi wa virusi alipochunguza kompyuta ya mteja wa Marekani yenye software ya kukinga virusi ya Kaspersky, aligundua kuwa kompyuta hii inatumia Windows feki, na imeambukizwa na kirusi cha “Equation“. Software ya kukinga virusi ilifanya kazi kama kawaida, na kutuma nyaraka zilizoambukizwa kirusi kwenda kwenye server ya Kaspersky ili zichambuliwe.
Baada ya kuona maneno ya “siri” kwenye nyaraka hizo, mchambuzi wa virusi aliripoti kwa Afisa mkuu mtendaji wa kampuni hiyo na Afisa huyo alimwagiza mchambuzi kufuta kabisa nyaraka hizo. Hivyo nyaraka hizo hakuna aliyenazo isipokuwa NSA wenyewe. Baadaye habari zikasema mtu anayemiliki kompyuta hiyo ni mfanyakazi wa NSA.