Kampuni mashuhuri ya utengenezaji rangi nchini ya Sadolin imenunuliwa na moja ya kampuni kubwa ya utengenezaji rangi Afrika na duniani, sasa kufahamika kwa jina la Kansai Plascon Tanzania.
Rangi za Sadolin zimejipatia umaarufu sana nchini, zimekuwa zikitengenezwa nchini kwa zaidi ya miaka 50. Kumbuka hadi lile neno la kikopo cha ‘kisado’ ambacho kwa sasa kinatumika kama kipimo limetokana na makopo ya rangi za Sadolin.
Ununuaji huo kwa ufupi:
- Jina la ‘Sadolin’ limekuwa likitumika kwa rangi za kampuni ya hapa Tanzania kwa leseni kutoka kampuni kubwa ya rangi ya AkzoNobel yenye makao makuu nchini Uholanzi.
- Viwanda vya utengenezaji wa rangi hizo kwa Tanzania na nchi za Jirani vimenunuliwa na kampuni kubwa nyingine ya Kansai Plascon Afrika na hivyo viwanda hivyo vitaacha kutumia jina la Sadolin kwenye bidhaa zake tena. Kuanzia sasa zitatambulika kwa jina la Plascon.
Kansai Paint ni kampuni ya aina gani?
- Kansai ni moja ya kampuni kubwa duniani pia kwenye eneo la utengenezaji na biashara ya rangi na makao makuu yake ni nchini Japani. Kansai inashika nafasi ya kumi duniani kwenye utengenezaji na uuzaji wa rangi.
- Kwa Afrika makao makuu ni Afrika Kusini na tawi la Afrika linajulikana kwa jina la Kansai Plascon.
Je viwanda vilivyokuwa vinatengeneza bidhaa za Sadolin vimenufaikaje?
Kwa kiasi kikubwa kampuni ya Kansai ina teknolojia kubwa katika maeneo ya utengenezaji rangi za matumizi mbalimbali nje tuu ya rangi za ujenzi. Inasemekana kwa Japan kampuni ya magari ya Toyota inatumia kiasi kikubwa cha rangi za Kansai kwenye magari yake.
Kwa kampuni iliyokuwa inafahamika kwa jina la Sadolin Tanzania, sasa Kansai Plascon Tanzania, itanufaika kwa teknolojia kubwa zaidi na pia bidhaa nyingi zaidi za rangi kulinganisha na zamani.