Unapokuwa umetumia kitu kwa muda fulani inafikia kipindi unakizoea hasa muonekano wake kiasi cha kwamba hata ukiona kwa mbali tu unaweza ukasema kwa uhakika kabisa kile ni kitu fulani.
Kama utakuwa ni mfuatiliaji mzuri wa programu mbalimbali utakuwa umeshasikia kuhusu muonekano wa giza kwenye programu zao mbalimbali, kwa uchache tu wengi wetu tunaweza tukawa tunafahamu kuwa unaweza kuchagua muonekano wa giza/mwanga kwenye Youtube. Mbali na hapo wakati fulani WhatsApp nayo ilielezwa kuwa kipengele hicho kitaongezwa.
Mwezi Oktoba mwaka jana (2018) ilielezwa kuwa Facebook Messenger itakuwa na uwezo wa kuwa na muonekano wa mwanga au giza lakini ni mpaka pale mtumiaji atakaporuhusu. Sasa kipengele hicho kimeruhusiwa ila sio waziwazi; inambidi mtu atumie ujanja fulani kuweza kuwasha muonekano wa giza kwenye Facebook Messenger.
Jinsi ya kuwasha muonekano wa giza kwenye FB Messenger
Itakubidi utume kikatuni cha mwezi (?) kwenye uwanja wa kuandika ujumbe kisha unatuma. Baada ya hapo litatokea neno ‘You Found Dark Mode!’, kisha chini yake kitatokea kitufe kilichoandikwa “Turn on in Settings” maana yake kwa tafsiri isiyo rasmi-‘Nenda kwenye mpangilio kuwasha’.
Vitu vingine huwa vinakuwepo lakini sio rahisi kuonekana machoni pa watu. Sasa kama wewe ni mpenzi wa muonekano wa giza ushindwe mwenyewe tu kuweka kwenye FB Messenger!
Vyanzo: XDA, Android Police, GSMArena