iPhone 8 Plus imeripotiwa kuwa na tatizo la betri unaosababisha simu hiyo kufumuka kwa kubanduka baina ya bodi na kioo cha simu hiyo.
Kwa mujibu wa mtumiaji wa nchini Taiwan aliyefahamika kwa jina la Bi Wu anasema simu yake iliachana wakati anaichaji.
Anasema alipoanza kuichaji ndani ya dakika tatu simu hiyo ilianza kufumuka kwa kujitenga baina ya bodi na kioo. Simu hiyo alikuwa ameinunua siku tano zilizopita. Simu hiyo tayari imepelekwa Apple kwa ajili ya uchunguzi.
Tatizo hilo halikumkumba pekee Ms Wu, mtumiaji mwingine wa kijapani alionesha katika ukurasa wake wa Twitter simu yake ya iPhone 8 Plus ikiwa katika boksi lake tayari imefumuka kabla ya kutumiwa.
Kabla ya watu kuwa na hofu ya iPhone 8 Plus hayo ni matukio mawili mpaka sasa yaliyoripotiwa. Hata hivyo sio jambo la kupuuzwa.
Bado hakuna maelezo ya kinachosababisha hali hiyo, lakini ripoti kutoka vyombo vya habari vya Korea Kusini zinaonesha kwamba betri ya iPhone 8 Plus ndio inayosababisha yote hayo. Kumeelezwa kwamba Betri inavimba na kusababisha hali hiyo ya kubanduka na kuachana.
Betri za simu za iPhone zimekuwa zikitengenezwa na kampuni za Samsung SDI na LG Chem ambao wamekuwa wakitengeneza kwa makampuni mengi ya uzalishaji wa Simu duniani.
Simu zote zilizoripotiwa kupatwa na tatizo hilo zimerudishwa kwa kampuni ya Apple kwa uchunguzi zaidi. Tusubiri tuone ripoti ya kutoka Apple inasemaje kuhusu matukio hayo na je kama kutakuwa na simu zingine zitakazopatwa na hali hiyo.