Siemens imeamua kuleta treni zinazo kimbia na zinazotumia injini ambazo zinatumia mafuta na umeme, uamuzi ambao unaingiza kampuni hii katika kundi la makampuni ambayo yanawekeza katika kutafuta usafiri wa kasi wa treni zaidi ya huu uliopo sasa.
Hii si mara ya kwanza kwa kampuni hii kutengeneza injini ambazo zinatumia mafuta na umeme, mwanzoni mwaka huu kampuni hii iliungana na Airbus kutengeneza injini kama hizi ila kwa ajiri ya ndege. Ni wazi kwamba Siemens wameona faida ama mwanga wa mafanikio katika sekta hii na ndio maana wameingia zaidi katika upande huu wa teknolojia.
Siemens imeendelea kuotesha mizizi yake katika sekta ya injini mchanganyiko kwa kuanza kutengeneza treni zitakazokuwa zinatumia injini zenye uwezo wa kutumia mafuta na pia umeme, kampuni hii itatengeneza treni kwa ajiri ya kampuni inayoitwa Brightline ambayo inaendesha mradi wa usafirishaji.
Katika kiwanda kilichopo California Marekani Siemens inatengeneza treni ambazo zinatumia injini zinazotumia mafuta na pia umeme, treni hii inategemewa kuwa na uwezo wa kwenda mwendo mpaka wa kilomita 200 kwa saa.
Hata hivyo ieleweke wazi kwamba treni hii sio treni inayokimbia zaidi, treni ya Shanghai Maglev ya huko Shanghai ndio inayokimbia zaidi. Shanghai Maglev ni treni inayotumia teknolojia ya usumaku na hukimbia mpaka kufika kilomita 430 kwa saa, huu ni mwendo wa kasi kweli kweli pengine ingekuchukua chini ya masaa matatu kutoka Dar es salaam hadi kufika Kigoma kwa treni hili.