Kampuni kubwa ya mawasiliano ya Telstra ya Australia mwanzoni mwa wiki hii imewasha teknolojia ya 5G ya majaribio yenye kasi zaidi kwa njia ya Wi-Fi.
Kampuni hiyo inakuwa ya kwanza kuwasha teknolojia ya 5G duniani na itapatikana bure katika michezo ya jumuiya ya madola (GC2018) itakayofanyika nchini humo kuanzia April 04 mpaka April 15 mwaka huu.
Teknolojia ya 5G itapatikana katika Pwani ya Gold coast, Queenslands ambapo michezo ya jumuiya ya madola itafanyika na wageni watakaohudhiria katika michuano hiyo watafurahia kupata intaneti ya bure na kusaidia kujaribu teknolojia mpya ya 5G.
Hata hivyo hakuna bado simu janja, Tablet au vifaa vinginevyo ambavyo vinaruhusu matumizi ya 5G. Kampuni ya Telstra imeweka idadi ya vituo vya Wi-Fi vinavyowezesha 5G ili kuweza kupima zaidi miundo mbinu yake mipya.
Telstra imetoa tahadhari kwamba kasi ya intaneti hiyo itatofautiana kulingana na vifaa vya watumiaji, umbali wa WiFi na mtumiaji na wingi wa watumiaji waliounganishwa kwenye Hotspot moja.
Wakati Telstra imeanza rasmi majaribio ya 5G huko Australia, Marekani kampuni za mawasilino za AT&T na Verizon zipo kwenye maandalizi ya kuanza teknolojia ya 5G.
AT&T imepanga kuanza teknolojia ya 5G katika miji 12 Marekani wakati Verizon wanashirikiana na Samsung kwa kuanzia huko Sacramento, California baadae mwaka huu.