Simu mpya inayotumia Harmony OS kutoka Huawei haitaingia sokoni mwaka huu. Kampuni hiyo inasema lengo lao ni kuendelea kutumia programu endeshaji ya Android.
Huawei tayari washatambulisha rasmi uwezo wa programu endeshaji yao wanayolenga kuitumia kama serikali ya Marekani watawekea vikwazo vya kuwazuia kutumia programu endeshi ya Android kutoka Google. Ni hivi karibuni tuu wameshatambulisha TV janja inayotumia programu endeshaji hiyo na pia wamesema wanatengeneza saa janja inayotumia programu endeshaji ya Harmony na kwamba itatambulishwa hivi karibuni.
Makamu wa Rais wa kampuni ya Huawei, Bwana Vincent Yangu alisema ‘Tunataka tuendelee kuwa sehemu ya utumiaji wa toleo moja la programu endeshaji na wadau wengine wote’, hapa akimaanisha Android.
Ameyasema hayo akiwa kwenye tukio moja jijini New York nchini Marekani. Kwa sasa inaonekana nia ya Huawei ni kuweka wazi kwa Marekani ya kwamba wanaweza kuendelea na biashara bila ya Android.
Bwana Yang amesema toleo la simu janja ya hadhi ya juu inayokuja, Huawei Mate 30 Pro, nalo litakuja na programu endeshaji ya Android. Uamuzi wa kuacha kutumia Android wataufanya haraka kama hali ya katazo la kibiashara dhidi yao litafanyika.
Bado tunaamini hadi kufikia mwakani tusishangae tukiona Huawei akitoa simu mpya inayotumia Harmony OS katika soko la China kwanza ili kuanza kulifanyia maboresho zaidi. Ni rahisi wao kuanza kwa China kutokana na watumiaji wa nchi kuwa rahisi zaidi kuiunga mkono kampuni ya nchini mwao.