Simu janja ya hadhi ya juu ya Huawei Mate 30 Pro inayotegemewa kuja hivi karibuni haitakuja na apps mbalimbali zinazomilikiwa na Google.
Kampuni ya Google imesema uamuzi huo umechangiwa na katazo kutoka serikali ya Marekani kwa makampuni ya nchi hiyo kufanya biashara na kampuni ya Huawei.
Simu hiyo inategemewa kutambulishwa rasmi mwezi wa tisa na uamuzi huu unaonekana utaathiri mauzo ya simu hiyo katika soko la kimataifa. Tayari simu janja za Huawei zilianza kufanya vizuri sana katika nchi za bara la Ulaya na kutokuwa na apps hizo muhimu wengi wanaamini mauzo ya simu hayo katika bara hilo yatakuwa madogo sana.
Apps za Google kama vile Google Maps, Google PlayStore, Google Search, Kivinjari cha Google, Gmail, na YouTube ni apps muhimu sana kwa watumiaji wengi wa sasa.
Umuhimu wa apps za Google unaonekana ata kwa watumiaji wa simu za iPhone ambapo apps za Google kama vile YouTube, Maps, Gmail, na Google Photos ni bado maarufu sana ingawa Apple ana huduma za namna hiyo pia.
Kwa nchini Uchina bado simu hiyo itaweza kufanya vizuri kwa kuwa huduma za apps za Google hazipatikani nchini humo kabisa. Na tayari huduma za app ya WeChat ndio huduma zinazoshikilia soko nchini humo na huduma hizo zitaendelea kupatikana kwenye simu zao za nchini humo.
Inasemakana kwa kutoa simu zisizokuja na apps za Google mauzo ya simu za Huawei yataporomoka kwa asilimia 40 hadi 60 (kulingana na jarida la Bloomberg). Tayari uongozi wa Huawei umesema suala hilo linaweza sababisha wao kupoteza mapato ya dola bilioni 10 kwa mwaka.