Kampuni ya Huawei yatambulisha rasmi toleo lao la simu janja za hadhi ya juu za Huawei Mate 30 na Mate 30 Pro, ingawa zinakuja na teknolojia za kisasa hii ikiwa ni pamoja na 5G ila haziji na uwezo wa kuwa na apps maarufu za Google.
Kupitia simu zake hizi mpya za Huawei Mate 30 na Mate 30 Pro itakuwa ni nafasi ya Huawei kujipima uwezo wao kama wanaweza kuendelea kutishia soko la simu janja za hadhi ya juu bila simu hizo kuja na familia ya apps za Google.
Kutokana na katazo la kibiashara liliwekwa na serikali ya Marekani kwa makampuni ya nchini humo, Google, Microsoft, Facebook na makampuni mengine mengi yaliyokuwa yakifanya biashara na Huawei yamejikuta yakikata uhusiano huo na hivyo kuzuia huduma zao kupatiakana kwenye simu au kompyuta mpya zinazotengenezwa na Huawei.
Je simu hii inakosa vipi vikubwa?
>Apps
Simu hizi zinakuja bila apps maarufu kama vile Google Playstore, Google Maps, Google Chrome, na zingine mbalimbali zinazomilikiwa na Google.
>Updates/Masasisho ya Google
Simu hii haitakuwa inapata masasisho muhimu ya kiusalama kwa wakati ukilinganisha na makampuni yanayokuja na toleo la Android kutoka Google. Kawaida inaweza kuchukua miezi kadhaa kabla ya masasisho ya kiusalama yaliyotengenezwa na Google kufikia toleo la bure la Android – ambalo ndilo Huawei anatumia kwa sasa.
>Kutokuwa na GMS (Google Mobile Services)
GMS – Google Mobile Services, ni teknolojia inayojumuhisha mfumo mzima wa kutumia teknolojia za kimawasiliano ndani ya simu. Kupitia teknolojia hii basi apps zinaweza kutumia vizuri teknolojia za mawasiliano zilizowekwa kwenye simu husika. Ata simu za China ambazo zimekuwa zikitengenezwa na kuuzwa nchini humo bila apps za Google bado zimekuwa zikitumia GMS ndani yake. Na hili limekuwa likifanya kuwa rahisi simu hizi kuwekwa apps za Google zikiuzwa nje ya China.
Simu za Huawei kuanzia sasa ikiwa ni pamoja na Mate 30 zinakuja na mfumo wa HMS – Huawei Mobile Services. Suala hili lina maanisha ata kama ukijaribu kuweka apps za Google kwa lazima – kwa kulazimisha kuweka Google Services (mfumo wa huduma za Google) bado itashindikana kwa kuwa mfumo huo unaohitajika kwa ajili ya apps za Google kufanya kazi hauendani na ule mfumo wa teknolojia mama ya kwenye programu endeshaji (yaani HMS).
Kutokana na hili ndoto ya simu hiyo kuweza kutumia apps za Google isahau.
Je soko la app la Huawei lina apps ngapi?
Kwenye simu hii kwa sasa bado kutakuwa na apps chache sana ukilinganisha na simu za Android ya Google. Hadi sasa soko la apps la kwenye simu hiyo lina apps 45,000 ukilinganisha soko la Google Playstore lina zaidi ya apps milioni 2.7.
Huawei wameweka bajeti kubwa kuwavutia watengenezaji apps kuhakikisha mfumo wake wa HMS unatambuliwa na apps zao ili ziweze kufanya kazi kwenye simu zake pia.
Sifa na uwezo wa Huawei Mate 30
- Inchi 6.53 OLED display
- Prosesa Kirin 990 CPU
- Uwezo wa kuzuia maji (water resistance)
- Kamera ina lensi tatu – megapixel 40, 16 na 8.
- Kamera ya selfi ni ya megapixel 24
- Uzito wa gramu 198 grams, na upana wa mm 8.8
- Betri la mAh 4,200
- Uwezo wa kuchaji wa bila waya (wireless charging).
- Programu endeshaji ya Android 10 (toleo la bure – open source)
- RAM ya GB 8, na diski ujazo wa GB 128.
Huawei Mate 30 Pro
- Inchi 6.62 OLED display
- Prosesa Kirin 990 CPU, 16-core Mali G76 GPU
- Uwezo wa kuzuia maji (water resistance)
- Kamera ya lensi tatu, hii ikiwa ni ya Megapixel 40, 40, 8.
- Kamera ya selfi ni ya megapixel 32- inasaidiwa na teknolojia ya kuboresha picha (AI HDR)
- Uzito wa gramu 198 grams, na upana wa mm 8.8
- Betri la mAh 4,500
- Uwezo wa kuchaji wa bila waya (wireless charging) na pamoja na kuweza kuchaji vifaa vingine kwa kutumia teknolojia hiyo.
- Programu endeshaji ya Android 10 (toleo la bure – open source)
- RAM ya GB 8, na diski ujazo wa GB 256, ila pia kuna uwezekano wa toleo la GB 512 kuja pia.
Simu zote zinakuja pia na teknolojia za USB Type C, mfumo wa mwasiliano wa 5G, uwezo wa kutumia Memori Kadi, na teknolojia zingine muhimu zilizozoeleka katika simu janja za kisasa.
Bei:
Huawei Mate 30 Pro itauzwa kwa $1,200, takribani Tsh 2,800,000/= huku Huawei Mate 30 ikienda kwa bei ya Tsh 2,000,000/=. Bei zitapanda kulingana na ujazo zaidi.