Programu endeshaji ya HongMeng OS inayotengenezwa na Huawei itatumika kwenye vifaa vingi zaidi ya simu tuu. Hayo yamesemwa na mkurugenzi mkuu wa Huawei katika mahojiano na chombo kimoja cha habari nchini Ufaransa.
Mwanzilishi wa Huawei, Bwana Ren Zhengfei amesema kupitia HongMeng OS hawafikirii suala la simu janja pekee, bali wanatengeneza programu endeshaji ambayo itaweza kufanya vizuri pia kwenye kompyuta, tableti na vifaa vingine janja vya kisasa vinavyoitaji programu endeshaji: mfano vifaa vya majumbani, magari n.k.
Katika mahojiano hayo na gazeti la Le Point Bwana Ren amesisitiza ya kwamba wanaangalia jinsi ya kupunguza utegemezi wao kwa kampuni ya Google.
Ingawa bado toleo la HongMeng OS halijaanza kupatikana rasmi ila kupitia majaribio wanayoyafanya tayari wamesema wanategemea programu endeshaji hiyo kuwa na utendaji wa kasi zaidi ikilinganishwa na Android na iOS. Ila bado ni mapema mno kuwa na uhakika usiopingika kwenye suala hili.
Huawei wanategemea programu endeshaji hii itakapokuwa tayari wataanza na soko la China, na kuwekeza katika utengenezaji apps kabla ya kuanza kuitumia kwenye simu zitakazouzwa katika mataifa mengine pia.