Inakwenda kwa jina la HarmonyOS. Kampuni ya Huawei imeweka wazi jina la programu endeshaji mpya kwa ajili ya simu na vifaa vya kisasa vya kielektroniki.
Jina la HarmonyOS ndio litafahamika duniani kote wakati kwa ndani ya China jina la Hongmeng OS litatumika.
Kampuni hiyo imesema programu endeshaji hiyo itatumika kwenye vifaa kama simu, spika na vingine vya kisasa vya elektroniki (internet of things).
#HarmonyOS was created with four major building blocks in mind, ensuring a new generation OS that is best suited for our digital world today. #HDC2019 pic.twitter.com/7vgEuwuUG6
— Huawei Mobile (@HuaweiMobile) August 9, 2019
Ni hivi karibuni tuu Huawei walisema bado watatumia Android kutoka Google ila wengi kwa sasa wanaamini wataanza kuleta simu kadhaa pia zikiwa na programu endeshaji yao.
Katazo la kibiashara la Marekani dhidi ya Huawei lilishalegezwa na Rais Trump ila inaonekana Huawei inaona ni bora ijiweke salama kabisa kwa kuwa na programu endeshaji yake iliyo huru dhidi ya vikwazo vya Marekani.
Programu endeshaji hii imetengenezewa apps mbalimbali kama vile za ramani (Maps), na nyingine muhimu na unazokutana nazo kwenye Android zikitoka Google au kwenye simu za iPhone zinazotengenezwa na Apple. Huawei imehakikisha kuna wingi wa apps mama.
Inasemekana programu endeshaji hiyo itaweza pia kutumia apps za Android. Tunaendelea kufuatilia maendeleo ya programu endeshaji hii ili kukupa habari zaidi pale zitakapotoka. Bado haijaonesha itakuwa na muonekano gani katika simu janja.