Wakati Marekani na Ufaransa wakifanya mazungumzo juu ya suala la kodi kwa makampuni ya biashara za kimtandaoni hasa hasa ya kimarekani tayari taarifa imetoka inayosema Google wamepigwa moja ya faini kubwa zaidi kuwahi kutolewa huko nchini Ufaransa.
Ni miezi sasa tokea serikali ya Marekani ipandishe kiwango cha kodi dhidi ya vinywaji vya divai (wine) vya nchini Ufaransa vinavyoingizwa Marekani, uamuzi huo ulikuja baada ya serikali ya Ufaransa kudai ya kwamba inataka kudai kodi nyingi kutoka kwa makampuni ya biashara za kimtandao kama Google, Facebook, Amazon na mengineyo.
Suala hilo halikupendwa Marekani kwa kuwa makampuni haya mengi ni ya nchini humo na huwa wanatoa ripoti zao za kifedha na kulipa kodi nchini Marekani na hivyo uamuzi wa Ufaransa unaweza kuwa kandamizi na kupunguza kodi kwa Marekani.
Wakati tayari serikali hizo mbili zimesema zitafanya mazungumzo kuhusu jambo hilo wachunguzi wa masuala ya kodi nchini Ufaransa wamefanikiwa kufikia makubaliano na Google yatakayohusisha kampuni hiyo kulipa zaidi ya dola bilioni 1 za Kimarekani (Zaidi ya Trilioni 2 za Kitanzania).
Google wamekuwa wakiendesha biashara za bara la Ulaya kutoka makao yao makuu ya barani humo yaliyopo Dublin nchini Ireland. Suala hili limewafanya wasiwe wanalipa kodi katika mengine, na sasa hali itabadilika sana kutokana na ushindi huu wa Ufaransa katika mazungumzo yake.
Biashara za mtandaoni zimekuwa zikikua kwa kasi sana na kitu kikubwa ni kwamba hazitambui mipaka ya nchi – ni utandawazi kwelikweli. Jambo hili linasumbua vyombo vingi vya kodi kwani malipo na biashara za kimtandao kati ya makampuni ya taifa moja hadi jingine yamekuwa yakikua kwa kasi.
Je una mtazamo gani juu ya suala hili?
Vyanzo: Reuters na vyanzo mbalimbali