Siku hizi sio kitu cha ajabu kabisa kuweza kununua na kufanya malipo bila hata kwenda dukani bali unatembelea dukani ukiwa mahali popote, wakati wowote na kufanya malipo bila wasiwasi wowote na masoko kama eBay yamekuwa msaada kwa watu wengi tu katika ulimwengu wa sasa uliotawaliwa na teknolojia.
Manunuzi kwa njia ya mtandao yamekuwa yakiboreshwa na kurahisishwa zaidi kadri miaka inavyozidi kusogea ambapo unaweza ukanunua vitu kiganjani mwako na kama wewe ni kati ya wale ambao tunapenda kununua vitu mtandaoni basi sina shaka utakuwa umeshathubutu kununua kitu kupitia tovuti ya eBay.
Kwa wale ambao hawafahamu eBay tovuti/programu tumishi/soko ambalo lina bidhaa mbalimbali zinazouzwa mtandaoni ambapo mtu akipenda bidhaa fulani anaweza akainunua papo hapo wa kufanya malipo kupitia PayPal, VISA, Mastercard, n.k kisha kusubiri baada ya siku kadhaa mzigo wako kukufikia iwapo nchi uliyopo wana huduma ya kutuma mzigo.
Kama njia ya kutanua wigo kwa wateja kufanya malipo eBay wataruhusu watu kuweza kufanya malipo kupitia Google Pay (G-Pay). Je, G-Pay ni nini? Google Pay ni mfuko wa kidijitali ulio chini ya Google unaoruhusu kutuma/kupokea pesa, kufanya malipo kwa njia ya mtandao. G-Pay ilizinduliwa Sept, 11 2015 na hapo awali uliitwa Android Pay lakini tangu Jan, 8 2018 jina lake lilibadilishwa na kuwa Google Pay.
Kuanzia mwezi Aprili kupitia eBay watu wataweza kufanya malipo kwa kutumia G-Pay katika mchakato wa kufanikisha kununua bidhaa na kisha kusubiri mzigo wako. Vipi wewe unaizungumziaje hatua ya Google Pay kuongezwa kwenye eBay?
Vyanzo: The Verge, CNET, ZDNet