Katika dunia ya leo suala la ulinzi katika ulimwengu wa utandawazi ni kitu ambacho makampuni ambayo yanajishughulisha na teknolojia yamekuwa yakijidhatiti siku baada ya siku na safari hii “Files ya Google” imeongezwa ubora.
Sote tunatumia vifaa vya Android toleo la kisasa ama wale ambao tunatumia Android Go tunafahamu vyema kuwa kuna programu tumishi iitwayo Files ndani ya rununu zetu mahususi kwa ajili ya kutunza vitu (picha, nyaraka, picha mnato, n.k) ambapo mtumiaji anaweza akafungua vitu alivyovihifadhi humo wakati wowote hata bila ya kutumia intaneti.
Mwaka 2017, “Files” ilionekana kwa mara ya kwanza kwenye toleo la Android Go huku ikilenga kumsaidia mtumiaji kuweza kupunguza vitu kwenye simu janja kiurahisi hivyo kufanya rununu kuwa na memori kwa matumizi mengineyo.
Sasa katika maboresho “Files ya Google” imeongezwa ulinzi wa kuweka faili waliloliita “Safe folder” ama faili salama (kwa mujibu wa tafsiri isiyo rasmi) ambapo mtumiaji ataweza kuweka ulinzi kwa kutumia nywila/nenosiri na itahitajika kila mara ambapo mtu atataka kukuona vilivyowekwa huko.
Pili, kwa chochote ambacho kitawekwa huko basi kitatoweka ile sehemu ambayo ilikuwa ikionekana hapo awali kulingana na aina ya kitu husika. Iwapo mtu mtu atataka kuona vitu vilivyofichwa atalazimika kuweka nywila kuweza kujua kilichomo ndani ya “Safe folder“.
Maboresho hayo kwa sasa yapo katika hatua ya majaribio ingawa yatapatikana katika siku za usoni. Tuambie mtazamo wako kuhusiana na hili ewe msomaji wetu unayependa usalama/faragha ya vitu vyako.
Vyanzo: Gadgets 360, The Verge