Facebook waunganisha uwezo wa kuchati Instagram na Facebook. Mara ya kwanza tuliandika kuhusu mpango wa Facebook kuunganisha uwezo wa kuchati na apps zingine za Instagram na WhatsApp mapema mwaka jana. Inaonekana tayari hatua za kuwezesha hilo zimefanikiwa.
Imeripotiwa tayari Facebook inafanya majaribio ya kuwawezesha watumiaji wa Instagram kuweza kuchati na marafiki zao wa Facebook moja kwa moja kwenye app hiyo bila kuhama. Yaani mmoja anakuwa anatuma meseji akiwa Instagram huku anayepokea anapokelea na kujibu akiwa kwenye app ya Facebook Messenger.
Jambo hili linaonekana ni maamuzi ya Facebook kuepuka hatua za kisheria za kulazimisha huduma hizo ziwe makampuni binafsi. Tayari kampuni hiyo ipo kwenye uchunguzi wa kiushindani – Inasemakana kwa Facebook kumiliki app ya Instagram na WhatsApp kunazuia huduma zingine kama hizo kukua/kushamiri.
Kwa kufanya hatua za kuunganisha Facebook wanataka kuonesha hizi zote ni huduma moja na hivyo kuja kufanya iwe vigumu vyombo vya serikali hasa vya bara la Ulaya au Marekani kulazimisha kampuni hiyo kujiondoa kwenye umiliki wa WhatsApp na Instagram.
Kwa sasa uwezo huo wa kutuma ujumbe wa maneno, video na picha baina ya watumiaji wa Facebook na Instagram umeanza kupatikana kwa baadhi ya watumiaji wake katika mataifa machache na ni muda wowote kuanzia sasa uwezo huo utasambaa kwa watumiaji wote duniani.
Watumiaji wa Facebook Messenger wataweza kupigiana simu za mfumo wa video na wakati huo huo kutazama video za Instagram kwa pamoja.
Hii ni hatua ya kwanza tokea Teknokona iripoti mapema mwaka jana kuhusu uwepo wa mpango huu. Wakuu wa huduma za Instagram na Messenger, Bwana Adam Mosseri na Stan Chudnovsky wamesema kwa kuunganisha huduma hizi watafanya huduma ya kuchati Instagram iwe bora zaidi kufikia vile ambavyo unaweza kuvifanya kwenye app ya Messenger.
Kujua kama una uwezo wa kufanya hivyo wamesema endelea kuhakikisha unatumia toleo la kisasa zaidi la Instagram kwa kusasisha app hiyo.
No Comment! Be the first one.