Vyanzo vya kuaminika vimevujisha taarifa zinazoonesha Facebook imekuwa ikishirikiana na China kutengeneza programu ya kompyuta itakayosaidia kuwachunguza watumiaji wa mtandao huo nchini China kwa niaba ya serikali hiyo.
Mark Zuckerberg amesifika kwa uamuzi wake wa kujifunza kichina na kuonesha jinsi gani amependa kujifunza kuhusu China ameshaenda nchini humo mara kadhaa na ata kukutana na viongozi wa taifa hilo ilihali mtandao huo maarufu bado umepigwa marufuku nchini humo.
Ni hivi karibuni tuu Zuckerberg alikuwa nchini China na alipata hadi muda wa kufanya mazungumzo na kiongozi wa taifa hilo, Bwana Xi Jinping.
Tokea mwaka 2009 mtandao wa Facebook umepigwa marufuku nchini China na njia pekee ya kutumia mtandao huo ni kupitia njia za kiudanganyifu zinazoonesha mtumiaji yupo nje ya taifa hilo.
Shirika la habari maarufu la New York Times limepata taarifa hizo nyeti kupitia wafanyakazi wa Facebook wa zamani na walio bado wakifanya kazi Facebook. Ingawa wamesema bado programu hiyo inafanyiwa kazi ndani ya kampuni hiyo bado hakuna maamuzi rasmi yaliyofanyika kuipa serikali ya China.
Inaonekana wazi ili kufanikiwa zaidi mtandao huo maarufu unaitaji watumiaji mamilioni kwa mamilioni wa intaneti waliopo nchini China. Kwa kiasi kikubwa haitashangaza kama taarifa hizi ni za kweli, imeshaonekana kwa kiasi kikubwa Facebook wanajitahidi kuona wanaweza kuelewana nini na serikali ya China ili kupata ruhusu ya tovuti hiyo kuweza kupatikana kwa watumiaji wa China.