Facebook waanza kuomba data za watumiaji wa iPhone baada ya Apple kuanza kuweka ulinzi mpya wa data za watumiaji wa simu za iPhone katika toleo la iOS 14.
Apple wameleta maboresho katika programu endeshaji ya iOS 14 inayotumika kwenye simu zake na tableti – maboresho yanayopigwa vikali na Facebook. Kupitia maboresho haya kwa sasa programu endeshaji itakuwa inazuia apps zingine kupata taarifa za utumiaji wa apps zingine na tovuti ambazo zinatembelewa na mtumiaji huyo wa simu.
Data hizi huwa muhimu kwa huduma za matangazo ya Facebook kwani ndio data ambazo zinaweza kuwaeleza sifa za mtumiaji wa simu husika – mfano kama una app nyingi za mambo ya mpira na huwa unatembelea zaidi tovuti za mpira basi ni kawaida kujikuta unatumiwa matangazo ya kubeti na mengineyo yanayohusisha vitu kama hivyo.
Apple wamesema wanafanya jitihada kulinda tabia data hizi za watumiaji wake wa simu dhidi ya matumizi mabovu yanayotajirisha makampuni mengine kama vile Facebook.
Kwa sasa watumiaji wa simu hizi watapewa chaguzi la kukubali au kukataa kuzipatia app zingine data muhimu pale watakapozifungua kwa mara ya kwanza. Facebook wanadai uamuzi huu utaathiri biashara nyingi hasa ndogo zinazotegemea kutangaza Facebook ili kupata wateja.
Uamuzi wa Apple ni mkubwa sana hasa kwa soko la Marekani ambapo watumiaji wa iPhone ni wengi sana. Suala hili litaathiri biashara ya Facebook kwa kiasi kikubwa. Je Google wanaweza kufanya jambo hilohilo? Ni vigumu kwani nao wanategemea sana biashara ya matangazo.
Vyanzo: CNBC na vyanzo mbalimbali
No Comment! Be the first one.