Bwana Elon Musk awa tajiri namba moja duniani na kushuka tena hadi namba 2 ndani ya muda wa siku chache. Kulingana na mahesabu ya jarida la Forbes, Bwana Elon Musk amepoteza utajiri wa zaidi ya dola bilioni 13.5 ndani ya siku chache na hivyo kupoteza nafasi ya kwanza.
Elon Musk ambaye ni mkurugenzi katika kampuni ya magari yanayotumia umeme ya Tesla na pia kwenye kampuni ya utengenezaji wa vyombo vya usafiri wa anga ya Space X alimpiku Bwana Jeff Bezos ambaye ameshikilia nafasi ya kwanza tokea mwaka 2017. Elon Musk alipewa nafasi ya kwanza Alhamisi iliyopita ila kufikia Jumatatu kampuni ya Tesla ilifanya vibaya sana kwenye soko la hisa na hivyo kushusha thamani za hisa za Elon Musk kwa zaidi dola bilioni 13.5 – alipoteza utajiri unaozidi Tsh Trilioni 13 kwa siku moja.
Je utajiri wa Elon Musk umetokea wapi?
Utajiri wa Bwana Elon Musk unapatikana zaidi katika umiliki wake wa hisa kwenye kampuni ya Tesla na thamani ya umiliki wake katika kampuni ya SpaceX. Ingawa Bwana Elon anajilipa mshahara mdogo katika makampuni hayo bado anapata utajiri mkubwa kupitia umiliki wa asilimia kubwa katika kampuni ya Tesla. Anamiliki takribani asilimia 21 ya kampuni ya Tesla – kumbuka kwa sasa kwa hadhi yake katika soko la hisa, kampuni ya Tesla ndio kampuni kubwa zaidi ya magari duniani kuyapita makampuni GM, Toyota na mengine mengi.
Kwenye kampuni ya SpaceX, bado kampuni haijaingizwa kwenye soko la hisa ila Elon Musk anaumiliki mkubwa kwenye kampuni hii pia. Data zinaonesha Bwana Elon Musk akiwa na umiliki wa asilimia 54 na huku asilimia zingine zikienda kwa mashirika na watu waliwekeza kwa makubaliano binafsi. Elon Musk hataki kuiingiza SpaceX kwenye soko la hisa mapema, hii ni ili kumuhakikishia kuendelea kuwa na nguvu kubwa katika kampuni hiyo, kumbuka ingawa ana umiliki wa asilimia 54, bado ameweza kubakia na asimilia 78 za ufanyaji maamuzi katika kampuni hiyo.
Kushuka kwa hisa za kampuni ya Tesla
Kampuni ya Tesla ina thamani ya zaidi ya dola bilioni 849 kwenye soko la hisa. Ukilinganisha na makampuni mengine ambayo tayari ni maarufu duniani ndipo utakapoona tofauti kubwa katika imani ya wawekezaji kwenye kampuni hii ya utengenezaji magari ya kisasa yanayotumia umeme.
Kampuni ya Tesla inaendelea kukua kwa kasi ikiwa na thamani ya takribani mara nne ukilinganisha na Toyota inayochukua nafasi ya pili kwa thamani ya uwekezaji kupitia masoko ya hisa.
Ingawa wengi wamejitokeza kuwekeza kwa kiasi kikubwa katika kampuni ya Tesla mwenyewe Elon Musk kwa muda mrefu amesema kampuni hiyo imepewa thamani kubwa sana kuliko inayostahili kwa sasa. Ingawa anaamini huko mbeleni itakuwa thamani hiyo ila kwa sasa anahisi nguvu ya soko umeifanya thamani ya hisa za kampuni hiyo kuwa juu kuliko uhalisia wake kwa sasa. Mfano ingawa tayari Tesla ilikuwa na thamani kubwa kuliko Toyota kwa mwaka 2019, Toyota waliuza magari mapya milioni 19.46 yaliyokuwa na thamani ya dola bilioni 281.2 kwa kipindi cha mwaka wa fedha ulioishia Machi 2020 – Tesla iliuza magari 367,200 yenye thamani ya dola bilioni 24.5 tuu.
Thamani za hisa za Tesla ziko juu kwani wawekezaji wengi wanaamini kampuni hiyo ndio itakayokuwa juu zaidi katika miaka ya mbeleni. Makampuni ya muda mrefu yameonekana kuwa nyuma zaidi kiteknolojia na hivyo wengi wanaamini yatapoteza nafasi zao sokoni.
Uwekezaji katika huduma ya intaneti ya kasi popote duniani
Nje ya teknolojia za safari za anga kupitia kampuni ya Space X Bwana Elon Musk analeta huduma ya intaneti ya kasi kupitia teknolojia za satelaiti itakayoweza kufikia eneo lolote duniani. Tayari wamesema wanategemea huduma hiyo itaundiwa kampuni nje ya Space X na itaingia kwenye soko la hisa. Uamuzi huu unaweza ongeza tena mabilioni ya dola ya utajiri kwa Bwana Elon Musk.
No Comment! Be the first one.