Mambo si mazuri kabisa kwa upande wa Facebook baada ya kukumbwa na kashfa inayopelekea watu kuanza kuukacha mtandao huo wa kijamii wenye watumiaji wengi ulimwenguni.
Mara tu Bw. Brian Acton ambaye ni mwanzilishi mwenza wa WhatsApp (hivi sasa WhatsApp ipo chini ya Facebook baada ya kununuliwa kwa $16bn) kuanzisha kampeni ya kufuta akaunti ya Facebook (#DeleteFacebook), sasa suala hilo ni maarufu sana kwenye Twitter inaonekana kupata mwitikio kutoka kwa watu wengi.
Elon Musk ni mmoja wa watu ambao wamefuta kurasa za SpaceX na Tesla zilizokuwa zimeshaidhinishwa (verified) baada tu ya mtu mmoja kumwambia “Afute kweli kama yeye ni mwanaume”.
Ni kitu rahisi sana kufuta ukurasa kwenye Facebook lakini ukweli ni kwamba Facebook wenyewe wamefanya imekuwa ngumu sana kuondoa kabisa ukurasa husika hata mara baada ya kile kipindi ambacho unaruhusiwa kurudisha tena ukurasa wako hewani kupita.
Elon Musk ameonekana mtu wa kutojali uwepo wa kurasa za mitandao ya kijamii kuhusu kile ambacho kampuni zilizopo chini yake zinazalisha. Pengine kujiamini huko kunatokana na alivyoweza kuibadilisha Tesla iliyokuwa ikionekana kampuni ambayo inaishia na kuibadilisha kabisa kwa kuifanya kuwa moja ya makampuni yenye uwekezaji mkubwa kwenye teknolojia.
Ni rahisi/vigumu kiasi gani kufuta ukurasa wa kwenye Facebook ambao unatumia/ulitumia muda mwingi kuujenga na kufikia mpaka hapo ulipo na ukizingatia kuna kashfa iliyoikumba Facebook?
Vyanzo: Gadgets 360, Vox
One Comment
Comments are closed.