Kutana na Ehang 184, drone ya kubeba abiria yaja. Teknolojia ya drone yazidi kuzidi kuboreshwa, kutoka upigaji picha, video, na sasa kubeba abiria.
Drone yenye uwezo wa kubeba abiria yafanyiwa majaribio huko Nevada, Marekani.
Utumiaji wa drones umeonekana kuuteka ulimwengu kwa kasi sana. Kwa mara nyingine watafiti wameendelea kuboresha uwezo wa drones kwani moja ya drones yenye uwezo wa kubeba abiria iliyotengenezwa na kampuni moja kutoka China “Ehang”imefanyiwa majaribio ya kubeba abiria na kufanikiwa.
Drone hiyo iitwayo “Ehang 184” yenye kutumia umeme ilijaribiwa ikiwa na abiria mmoja na kusafiri kwa zaidi ya dakika 20.
Drone hiyo ina mota 8 ambazo hata kama moja ikiwa na matatizo bado itaweza kutua bila matatizo, inachajiwa kwa saa 2 mpaka 4, imeundwa kuweza kubeba mzigo wa takribani kilo 100 na ina uwezo wa kwenda kwa kasi ya hadi wastani wa Km 100 kwa saa.
Ili kuweza kupaa au kutua drone hiyo abiria anatakiwa kuiamuru. Kutakuwa na kifaa cha tableti na atatakiwa kubofya kuamuru kuanza kupaa na kuelekea anapokwenda, na ikifika eneo husika lazima kubofya kuiruhusu kutua.
Uwepo wa abiria katika drone hiyo ni kwa sababu kuu mbili: Kuweza kuiamuru wapi impeleke na kuimamuru kutua wakati imefika ilipoamuliwa kwenda.
Kama tatizo likitokea abiria huyo hana uwezo wa kusaidia kuhakikisha inatua salama hivyo basi kampuni wamehakikisha kuwepo kwa vituo vya msaada ambavyo kazi yake ni kuhakikisha drone hiyo itatua salama kama ikipata itilafu wakati wowote.
Drone hiyo inatarajiwa kuuzwa kati ya dola 200,000 za Kimarekani mpaka dola 300,000 za Kimarekani. Kwa hakika teknolojia ya drones inayokuwa kila leo inazidi kuvutia wengi na kufanya kupendwa na wengi.
Chanzo: theguardian, live science