Watafiti wa Taasisi ya Utafiti wa wanyamapori Tanzania wakishirikiana na Mradi wa Tembo wa Mara wamekuwa wakitumia Drones kusaidia kuwalinda tembo wasitoke katika mipaka ya hifadhi na kwenda katika vijiji vya jirani.
Utafiti huu ambao kama utafanikiwa basi itakuwa ni hatua kubwa katika harakati za kulinda na kukuza idadi ya tembo nchini.
Tayari wanyama hawa wapo katika hatari ya kutoweka katika dunia kutokana uwindaji haramu uliokithiri, ukweli ni kwamba pamoja na ujangiri tembo wengi hufa kila mwaka baada ya kuvamia mashamba ya vijiji jirani na hifadhi.
Kwa mujibu wa watafiti hawa ni kwamba kelele za drone zinatosha kuwarudisha tembo katika maeneo salama bila ya kutumia nguvu kubwa, utafiti huu tayari umeonesha mafanikio makubwa na matokeo yake yamechapishwa katika chapisho la kisayansi.
Yajue baadhi ya Tabia kuhusu wanyama hawa ambao wanalindwa wasije kupotea kabisa.
- Wanasifika kwa kuwa na uwezo mkubwa wa kumbukumbu na hii ndiyo inasemwa kwamba huwasaidia viongozi wa makundi kuweza kukumbuka sehemu maji yalipo kipindi cha kiangazi.
- Hubeba mimba kwa miezi 22 na wakizaa huzaa mtoto mmoja tu (mara chache sana hupata mapacha), mtoto wa tembo akizaliwa inamchukua miezi kadhaa kuanza kuweza kuutumia mkonga wake na katika kipindi hiki hutumia mdomo kunyonya.
- Pamoja na kwamba uwindaji haramu unatishia uwepo wa wanyama hawa lakini tishio kubwa zaidi ni mabadiliko ya hali ya hewa ambayo yatasababisha kutoweka kwa mazingira ambayo watoto huweza kuishi, hii inamana mabadiliko ya hali ya hewa yatasababisha watoto wasiweze kufikia umri wa kuzaliana.
- Zipo aina mbili za wanyama hawa, wale wanaopatikana katika bara la Asia na wanaopatikana katika bara la Afrika
- Wanyama hawa huwasiliana kwa vishindo ardhini ambavyo husafiri kwa kasi kubwa kushinda sauti inavyosafiri katika hewa.
Kumbuka kusambaza makala na pia kuungana nasi kupitia Facebook, Twitter, Instagram, YouTube, Telegram na Google Plus