Hivi sasa ukenda kwenye maduka ya Samsung utakutana na simu janja Samsung Galaxy Note 9 ambayo ilitoka mwezi Agosti 2018. Mwaka huu tayari taarifa mbalimbali zimeshaanza kuenea kuhusu toleo lijalo kutoka familia ya “Galaxy Note”.
Ni karibu miezi kenda (9) imepita sasa tangu dunia ifahamu rasmi kuwa kuna Samsung Galaxy Note 9 kwenye soko la ushindani na kwa hakika hutaweza kuacha kuiongelea simu huika kutokana na sifa lukuki ambazo ni kivutio katika teknolojia ya leo lakini hilo sasa imebaki kuwa historia kwani Samsung Galaxy Note 10 na 10 Pro zinapiga jaramba tayari kwa kuletwa machoni pa watu.
Ingawa bado rununu (simu janja) husika hazijatoka lakini sio kitu cha kushangaza katika dunia ya leo kuweza kupata dondoo kuhusu bidhaa husika na yale ambayo yanakuwa yalikwishafahamika tangu hapo awali yanakuwa hayatofautiani na sifa za bidhaa husika wakati wa uzinduzi rasmi. Machache ambayo yamefahamika kuhusu Samsung Galaxy Note 10 Pro ni kama ifuatavyo:-
Kipuri mama. Innategemewa kuwa wakati wa uzinduzi wa simu kutoka familia ya Galaxy Note Samsung watazindua simu mbili kwa mara moja (Samsung Galaxy Note 10 na 10 Pro) ambazo zitakuwa na Exynos 9820 na Snapdragon 855.
RAM. Upande wa RAM inaelezwa tutegemee kuona Galaxy Note 10 Pro ambayo itakuwa na GB 6 za RAM; kuhusu memori ya ndani bado haijafahamika.
Uwezo wa betri. Kuhusu betri lake litakuwa na uwezo gani hapa ndio Samsung wamefanya vitu vikubwa na kwa taarifa simu husika itakuwa yenye teknolojia ya kuchaji haraka zaidi kuliko simu nyingine yoyote kwani inaelezwa kuwa na 25W, mtangulizi wake-Galaxy Note 9 ana 15W na kwa ujumla beteri lake linaelezwa kuwa na 4500mAh.
Kwa kuhitimisha dondoo inaaminika kabisa Samsung watatoa Galaxy Note nayotumia 4G na nyingine ya 5G lakini pia ule upnde wa kamera za nyuma utakuwa na maboresho/mabadiliko makubwa ingawa hakuna sifa za ndani kuhusu kamera zake zitakavyokuwa.
Vyanzo: Android Headlines, GSMArena