Data za akaunti milioni 210 za watumiaji wa mtandao wa Facebook zavuja baada ya kudukiliwa na taarifa za akaunti zao zinapatikana kwa urahisi mtandaoni.
Jumla ya data zilizowekwa wazi zinaonesha ni data zinazohusisha akaunti milioni 419 ila msemaji wa Facebook amesema baada ya kuzipitia wamegundua ni milioni 210 tuu na huku akidai data hizo nyingi zake ni za akaunti za zamani, na nyingine zimerudiwa – zinahusisha akaunti zile zile.
Data hizo zimehusisha taarifa muhimu kuhusu watumiaji wa Facebook kama vile anuani za akaunti zao, namba zao za simu na pia kwa baadhi ni majina yote ya muhusika.
Data hizo zimehusisha watumiaji wa Marekani zaidi – ambapo akaunti milioni 133 kati ya 210 zilikuwa za watumiaji wa nchi hiyo. Huku milioni 50 zikiwa za watumiaji kutoka Vietenamu, huku milioni 18 zikiwa za Waingereza. Udukuzi huu umechukua sifa ya kuwa moja ya udukuzi mkubwa zaidi wa data duniani – kwa idadi ya watumiaji.
Tayari Facebook na makampuni mengine makubwa ya kimtandao kama vile Google na Amazon wamejikuta kwenye hali ya kuangaliwa kwa jicho la ukali na umakini zaidi na vyombo vya usalama wa data za watumiaji wa huduma zake. Vyombo vya serikali ya Marekani na ata barani Ulaya zishazipiga faini kubwa kwa ukiukwaji wa usalama wa data za watumiaji wa huduma zao. Umoja wa Ulaya (EU) umetoa onyo kali baada ya taarifa hizi kutoka, uchunguzi unaweza kufuata.
Taarifa hii imekuja wakati mbaya kwani tayari Facebook wanapata pingamizi la kiaina kutoka bunge la Marekani (Congress) kuhusu wazo lao la kuja na sarafu yao ya kidigitali – libra. Kama hawawezi kulinda data za watumiaji wao wa mtandao wa kijamii kama Facebook inaweza ikawa hatari kupewa nafasi katika sekta ya fedha.
Tayari bunge la Marekani limeandaa mswada unaokwenda kwa jina la ‘Keep Big Tech Out of Finance Act’, yaani ‘Kuweka makampuni makubwa ya sekta ya teknolojia nje ya sekta ya fedha’ – lengo likiwa ni kuyazuia makampuni kama Google, Facebook na Amazon kuingia kwenye sekta ya huduma za kifedha.