Kampuni ya utengenezaji ndege ya Boeing ya nchini Marekani yaamua kuendelea na utengenezaji wa ndege za 737 Max. Kampuni hiyo ilifunga kiwanda hicho kwa kipindi cha miezi kadhaa sasa, ndege za 737 Max ni ndege ambazo zimepigwa marufuku kuruka kwa sasa kupisha uchunguzi unaoendelea.
Kiwanda hicho kilichopo katika jiji la Seattle ndio kinahusisha uundwaji na utengenezaji mzima wa ndege hizo unaohusisha pia utumiaji wa vipuli vinavyotoka maeneo mbalimbali.
Ndege za 737 Max zilipigwa marufuku duniani kote kutumika kwa sasa hadi hapo uchunguzi wa usalama wa ndege hizo utakapokamilika baada ya ajali mbili kutokea mapema mwaka jana na kusababisha vifo vya zaidi ya watu 346.
Boeing wamesema wametumia muda ambao walikifunga kiwanda hicho kwenye kuwekeza katika kuboresha usalama na ubora wa utengenezaji wa ndege hizo. Inawezakana pia wamefanya uamuzi huu wakiamini ndege hizo zitaruhusiwa kufanya kazi tena baada ya uchunguzi kukamilika.
Kuna taarifa zinaonesha ndege hiyo inaweza kuruka tena mwisho wa mwaka huu, ikitegemewa mabadiliko makubwa ambayo Boeing atakiwa kuyafanya kwenye ndege hizo yanahusisha mfumo wake wa kompyuta na mafunzo kwa marubani.
Ndege za 737 Max ni ndege zilizoanza kuuzika kwa kasi na Boeing ana oda ya zaidi ya ndege 3,800 kutoka kwa makampuni mbalimbali ya ndege duniani kote.
Makampuni haya yanaweza kuziamini tena ndege hizi ila swali je wasafiri wataweza kuziamini tena? Tayari chama cha wahudumu wa ndege nchini Marekani wamesema watataka kupata uhakika wa hali ya juu kuhusu usalama wa ndege hizo, wanachama wake wamelalamika kwamba hawataweza kufanya kazi kwa amani kama watalazimishwa kuhudumia ndege hizo bila uhakika mzuri wa kwamba tatizo lililosababisha ajali zingine limetatuliwa.
Kusimamishwa kwa utengenezaji wa ndege hizi pamoja na janga la Corona kusababisha biashara ya usafiri wa ndege kuathirika sana kumesababisha ajira 6,770 kupotea nchini Marekani kwenye kampuni ya Boeing. Na wamesema wanategemea hali kujitokeza pia kwenye ofisi na viwanda vyake vingine katika mataifa mengine.