BlackBerry yapata faida. Kwa kipindi cha miaka mingi hivi karibuni kampuni ya BlackBerry imekuwa na majanga ya kupata hasara za mfululizo hali iliyosababisha kampuni hiyo iliyokuwa nguli kwenye biashara ya simu kupoteza asilimia kubwa ya thamani yake.
Alhamisi hii kampuni hiyo ya nchini Canada imetangaza taarifa ya mapato ya kipindi cha robo mwaka kilichopita kinachoonesha kampuni hiyo imepata faida nzuri kuliko ilivyokuwa imetarajiwa hasa hasa kwenye biashara yake ya huduma za teknolojia – software.

Katika kipindi cha pili cha robo mwaka kilichoishia Agosti 31 mapato katika kitengo cha teknolojia na huduma (Software and services) kilipata ukuaji wa mapato kwa asilimia 26, mapato yalifikia dola milioni 196 za Marekani.
Kampuni ya BlackBerry chini ya mkurugenzi wake Mr Chen imeweza kubadili mfumo wa kibiashara yake, iliachana na kuhusika moja kwa moja na utengenezaji simu baada ya kuendelea kupata hasara kwa miaka mingi na ikaamua kujikita zaidi katika utengenezaji wa teknolojia na huduma mbalimbali za kiusalama katika eneo la teknolojia.
Kwa sasa kampuni ya nchini Uchina, ya TLC ndiyo inayohusika na utengenezaji wa simu zinazobeba jina la BlackBerry. Kampuni ya BlackBerry inaingiza mapato kwa kila simu inayobeba jina hilo, ila pia wanahusishwa kwa kiwango flani katika ubunifu wa simu hizo.