Wamejaribu…wakashindwa…..wakajaribu tena na wakashindwa. Wakaja na Android na bado imeshindakana. Sasa ni rasmi, BlackBerry waachana na biashara ya utengenezaji simu janja.
Mkurugenzi Mkuu (CEO) wa kampuni ya BlackBerry Bwana John Chen amejaribu mara kadhaa kuja na simu mpya tokea aanze kuongoza kampuni ya BlackBerry mwaka 2013.
Kwa wakati huo huo alianza kuongoza misuli ya kampuni hiyo katika biashara za teknolojia za kiusalama na ulinzi zaidi (mobile and security software & apps) lakini inaonekana ingawa bado wanauwezo mzuri wa kuendelea kutengeneza faida katika eneo la teknolojia za kiusalama (security softwares), biashara ya utengenezaji simu imekuwa ikiwavuta chini.
Inasemekana Mkurugenzi huyo alijipa hadi Septemba mwaka huu kuona kama biashara yao ya utengenezaji simu itaanza kutengeneza faida kabla ya kufanya uamuzi juu ya biashara hiyo. Kufikia Septemba mwaka ingawa tayari wametambulisha simu janja kadhaa zenye ubora mzuri bado hawakufanikiwa kufanya vizuri sokoni.
Bwana Chen amesema soko la simu limejaa ushindani mkubwa sana kutoka makampuni mengi sana kiasi cha kwamba ni vigumu wao kufanikiwa kila walipojaribu kuingia.
Ila kitu kikuu ni kwamba ingawa wenyewe wanaachana na biashara ya kutengeneza na kuuza simu zinazobeba jina lao wapo tayari kutoa leseni kwa kampuni nyingine kujihusisha na utengenezaji na uuzaji wa simu zinazobeba jina la BlackBerry. Kutoa ruhusa hii kwa mfumo wa leseni za kibiashara utahakikisha wanaendelea kunufaika na uuzwaji wa simu zinazotumia jina la BlackBerry.
BlackBerry watajikita katika utengenezaji na uuzaji wa ‘softwares/programu’ za kiusalama dhidi ya udukuzi wa kimtandao.
Biashara ya simu janja za BlackBerry ilianza kupata upinzani kutokana na ujio wa simu za iPhone mwaka 2007 na ujio wa simu ya kwanza inayotumia Android mwishoni wa mwaka 2008. Ukuaji mkubwa wa ushindani kutoka simu za iPhone na Android, pamoja na uchelewaji wa kufanya mabadiliko na maboresho muhimu ya kiushindani katika simu zao na biashara yao ndio kilicholeta majanga kwa kampuni hiyo.
One Comment
Comments are closed.