Katika dunia ya leo ni kitu cha kawaida mtu kuweza kununua kitu kupitia mtandao na akakipata baada ya muda mfupi lakini unafahamu ni lini mtindo huo ulianzishwa?
Karibu robo karne iliyopita kufanya biashara mtandaoni (kuuza/kununua kitu kwa njia ya intaneti) ilikuwa ni kitu haramu na kisichokubalika na mamlaka husika.
Historia inaeleza kuwa kati ya mwaka 1971 na 1972 wanafunzi wa chuo kikuu cha Stanford na wengine kutoka MIT walipanga kufanya biashara ya bangi kupitia ARPANET–hii ilikuwa mbinu ya mapema sana ya kufanya mawasiliano ambayo baadae ilileta TCP/IP. Lakini hii haikuwa biashara ya kwanza kufanyika mtandaoni bali yanachukuliwa kama maelewano tuu.
Agosti, 11 1994 ndio siku ambayo biashara ya kwanza mtandaoni ilifanyika kwa sababu Bw. Dan Kohn (alitengeneza tovuti iitwayo NetMarket) alishuhudia rafiki yake kutoka Philadelphia akiweza kununua CD ya muziki kwa $12.48 pamoja na gharama za kumfikia.
CD hiyo ilinunuliwa kupitia tovuti ya NetMarket na kutumia programu wezeshi kuweza kuficha namba za kadi ya akaunti yake ili hata N.S.A wakijaribu kufuatilia muamala umefanya na nani wasiweze kujua.