Apple kuzibania apps za Facebook, WhatsApp na apps nyingine mbalimbali kwenye iPhone katika uamuzi unaoonesha kuziathiri apps nyingine nyingi.
Apple wamesema wanafanya mabadiliko katika teknolojia ya simu zinazotumia internet (voice over internet protocol – VoIP). Katika mabadiliko hayo programu endeshaji ya iOS haitaruhusu apps zisizotumika kuendelea kufanya kazi nyuma ya pazia (background) kwenye iPhone.
Apps zinazotumia teknolojia ya simu kwa njia ya intaneti kama vile Facebook na WhatsApp huwa zinaitaji apps hizo ziendelee kufanya kazi ata kama mtumiaji wa simu hazitumii kwa wakati huo.
Uamuzi huu wa Apple inasemekana umejikita zaidi katika suala la kulinda faragha ya watumiaji wa simu zake. Inasemekana bado apps hizo zikiwa zinafanya kazi nyuma ya pazia zimekuwa zikikusanya data kuhusu utumiaji wa simu wa mtu husika, na kwa kufanya hivi Apple wanaamini watazuia jambo hilo kufanywa na apps za namna hii.
Mabadiliko hayo yatakuja kwenye toleo la iOS 13 linalotegemewa kutambulishwa rasmi mwezi wa tisa mwaka huu. Watengenezaji apps wamepewa hadi Aprili 2020 kuhakikisha apps zao zinafuata utaratibu huu mpya.