Ukipokea pesa kwa njia ya simu kimakosa ni bora kuzirudisha kwa aliyekutumia au unaweza jikuta katika mikono ya sheria na kuishia kulipa pesa nyingi zaidi.
Mwanamke mwenye umri wa miaka 45 amepigwa faini ya Shilingi za kenya 40,000(sawa na shilingi za kitanzania 866,248) na mahakama ya Embu au atumikie kifungo cha miezi sita gerezani kwa kukataa kurudisha Shilingi za Kenya 27,140 (sawa na shilingi za kitanzania 587,749) alizotumiwa kupitia kwa M-pesa kimakosa.
Bi Margaret Njeri alipatikana na hatia ya kukataa kurudisha pesa hizo alizopokea kutoka kwa Bw Richard Mbui katika eneo la Muthatari, kaunti ndogo ya Embu Magharibi.
Hakimu Mkazi wa Embu, Bi Julian Ndengeri, alielezwa jinsi Bw Mbui alivyotuma pesa kiasi cha shilingi 27,140 za Kenya kimakosa.
Bi Njeri alizitua pesa hizo mara moja baada ya kuzipokea na kisha akaanza kutopokea simu za Bwana Mbui.
Bw Mbui aliripoti kituo cha polisi ambapo wapelelezi walianzisha msako mara moja kwa kufuatilia maeneo ambako simu ya Bi Njeri ilikuwa ikielekea.
Akitoa hukumu yake, Bi Ndengeri alisema ushahidi uliowasilishwa mahakamani ulithibitisha kuwa Bi Njeri aliiba pesa hizo.