Mdukuzi mmoja Marekani adukua mfumo wa maji wa jiji la Oldsmar kwenye jimbo la Florida na kutaka kuongeza kiwango cha kemikali kwenye maji hayo ili kuyafanya kuwa hatari kwa afya ya binadamu.
Tukio hilo limewekwa wazi tarehe 9 Februari na uongozi wa jiji hilo, na wamesema tukio hilo lilitokea Ijumaa tarehe 5 mwezi huu.
Mifumo mingi ya kisasa ya huduma muhimu kama umeme na maji tayari imehusishwa kuunganisha katika mfumo wa intaneti ili kuruhusu uendeshwaji na ufuatiliaji wa karibu kutoka kwa wasimamizi wa chini hadi wa ngazi za juu – hii ni kwa mataifa mengi yaliyoendelea. Ingawa kiusalama uwezo huo unakuwa unahusisha watu wanaoweza kuingia kwenye programu spesheli ya usimamizi ila wadukuzi wanakuwa wanalenga kompyuta zenye programu hizo za uendeshaji wa mitambo.
Katika siku hiyo ya Ijumaa asubuhi ya saa 2 mdukuzi huyo alidukua mifumo ya kompyuta ya inayosimamia uendeshaji wa mitambo ya maji safi na kuweza kuwasha mfumo wa kubadilisha vipimo vya kemikali ya maji kupitia njia za kidigitali.
Akaingia tena mchana wa saa saba na nusu na kuanza kufanya mabadiliko ya viwango vya kemikali, na ndipo mfanyakazi aliyekuwa anaangalia kompyuta hiyo akatambua kwa kuona mshale wa kipanya (mouse) ukiwa unafanya mabadiliko wakati ofisini hapo hakukuwa na mtu anayeitumia kompyuta hiyo.
Inasemekana alikuwa anaongeza kiwango cha kemikali ya ‘Sodium Hydr0xide’, kemikali hiyo huwa inawekwa kwa kiwango kidogo ili kusaidia kusafisha maji – mdukuzi huyo alikuwa anakiongeza kiwango kutoka 100 hadi 11,000 – ongezeko ambalo lingeleta madhara makubwa kiafya kwa mtu yeyote ambaye angetumia maji hayo.
No Comment! Be the first one.