Kwa mtu ambae intaneti ni sehemu kubwa ya maisha yangu kwa sasa – kupata huduma ya intaneti nje ya kazini yenye kunihakikishia kasi nzuri na kwa gharama nafuu imekua ni pambano la muda mrefu.
Katika safari hiyo nimeshajikuta nikitumia vifaa na bando za mitandao karibia yote, nimeshamiliki modemu na Mi-Fi/router (vifaa vya WIFI) vya TTCL, Airtel, Tigo, Vodacom, Smile na hata Smart (Smart kwa kipindi fulani walikuwa wadau wa Teknokona).
Hapa naongelea nje ya intaneti ya kwenye simu yangu – kwenye simu kwa sasa natumia mtandao wa Airtel na Tigo (Namba ya Tigo nilihama mtandao kutoka Halotel) -> Fahamu jinsi ya kuhama mtandao bila kubadili namba yako ya simu.
Mwaka jana nilitumia sana Vodacom kabla ya kujua ya kwamba eneo ninaloishi limefikiwa na huduma ya intaneti ya Zuku Fiber. Kwa muda mrefu tayari nilikuwa nafahamu huduma ya Zuku Fiber kupitia eneo langu la kazi – ambapo ni ya kasi na haina ‘downtimes’ (muda ambao huduma inasumbua) sana kama huduma zingine tulizokuwa tunatumia kabla.
Baada ya kufahamu intaneti inaweza kunifikia eneo la Msasani ninaloishi basi niliulizia gharama za kuunganishwa – jibu likawa ‘Kuunganishwa ni BURE’ yaani ufundi + vifaa vya waya kwa hii teknolojia ya fiber+ router (kifaa cha wireless). Vyote hivyo ni bure ninachotakiwa tuu ni kulipia kifurushi cha mwezi.
Katika vifurushi kwa ajili ya majumbani Zuku Fiber wanaanzia Tsh. 69,000/= (hiki kinakuja na intaneti tu), pia kuna cha Tsh. 79,000/= kwa wale wanaotaka kupewa pia king’amuzi ambacho kinaunganishwa na mfumo huo huo wa intaneti – yaani hakuna kutumia ungo.
Huduma yao imekuwa ya uhakika hasa kwa mtu ambayo nategemea intaneti kwa huduma zote za ‘entertainment’ nyumbani – TV ikiwa inakuja na apps za Netflix na YouTube. Pia nikiwa nimeunganisha kompyuta moja ya ‘desktop’ spesheli kwa ajili ya programu nzito hii ikiwa ni pamoja na magemu. Intaneti ni huduma ambayo siwezi kuishi nayo.
Zaidi ya miezi 4 baadae naweza kusema huduma imekuwa ya kiwango na ubora wa juu sana, hii ni pamoja na uwezo wa kuangalia video za ubora wa HD ya 4K bila kusubiri mambo ya ku’load’. Kila kitu ni kubofya tu nacho kinafanya kazi moja kwa moja.
TATIZO: ‘Huduma ya wateja pale tatizo linapotokea’..
Miezi kadhaa nyuma, kuna siku ilidondoka mvua kubwa sana kipindi cha wikiendi. Na ghafla huduma ya intaneti ikakosekana asubuhi yake, nikatoa ripoti jumatatu yake kwa njia ya simu – Huduma kwa wateja wikiendi au baada ya saa 2 si ya uhakika.
Ilichukua zaidi ya wiki kwa tatizo langu kutatuliwa, watu wa huduma za matengezo kwa kutembelea nyumbani hawakuwa katika ubora mzuri – ‘professional’ hasa kwenye tabia na ufuatiliaji. Muda ambao niliwapa wa kuja nyumbani – kwa kuwa ni katikati ya wiki, hawakutokea. Hili suala lilinipa hasira hadi nikaamua kuandikia barua pepe (email) kitengo kikuu cha huduma kwa wateja – sikupata majibu.
Baada ya siku kadhaa nikaamua kufanya mawasiliano mengine na nikadai kurudhishiwa zaidi ya wiki ya kutokuwa na huduma – mtu wa kutengeneza alifika kwangu na kurekebisha na huduma ikarudi. Ila cha ajabu ingawa nilipewa ahadi ya kurudishiwa zaidi ya siku 5 – 7 ambazo sikuwa na huduma hili halikufanyika hadi leo hii.
Web portal: Huduma ya akaunti ya kimtandao ya Zuku Fiber inaonekana imetelekezwa. Bili zinaripotiwa kwenye shilingi ya Kenya (Ksh) badala ya Tanzania (Tsh), na bado eneo la mawasiliano pia utapatiwa mawasiliano ya Kenya badala ya Tanzania.
Ila bado Zuku Fiber ni chaguo zuri…
Zuku Fiber ni huduma ambayo ni ya bei nafuu sana na yenye kiwango cha juu cha kasi ya intaneti. Ila Zuku wanatakiwa waboreshe mifumo ya huduma kwa wateja, huduma kwa wateja si kuwa na namba ya kupiga tuu – huduma kwa wateja iliyo bora ni jinsi gani watakuwa na uwezo wa kufanya ufuatiliaji wa karibu wa matatizo ya wateja wao.
TCRA wanatakiwa wafanye kampeni kubwa kuhusu haki za wateja, ingawa nililipia huduma ya wiki 4 (mwezi) na nikakaa wiki nzima bila huduma ambayo sikuweza kurudishiwa siku hizo kwenye bili yangu bado sina uhakika kama haki yangu hii inaheshimika na ni haki ambayo naweza kuidai kwa hatua za kisheria dhidi ya Zuku.
Kwa sasa Zuku Fiber wanatoa huduma maeneo ya Masaki, Msasani, Kariakoo, Mikocheni. Sina uhakika wa maeneo mengine zaidi.
Nje ya hapo nikilinganisha na huduma nyingi za intaneti zilizopo, kwa maeneo ya majumbani, kama mtu anaweza kupata huduma ya Zuku Fiber basi hakuna huduma nyingine inayoweza kushindana nayo kwa sasa. Kupata tatizo la huduma mara moja ndani ya miezi 4 ni kiwango kikubwa cha ubora wa huduma husika, ila bado wanatakiwa kuboresha jinsi huduma kwa wateja inafanya kazi pale mteja anapopata shida na huduma yao.