Simu ya mkunjo wa display inakuja hivi karibuni. Kuanzia mwisho wa mwaka 2018 tumeona mabadiliko makubwa katika ubunifu wa simu katika eneo la kamera. Tumeona eneo la display/kioo likizidi kujaa katika uso wote wa simu, kwa 2019 inaonekana utakuwa mwaka wa display/vioo vya mkunjo.
Samsung tayari wameshatangaza watambulisha simu yenye display/kioo cha mkunjo na sasa kampuni ya simu inayokua kwa kasi zaidi kwa sasa duniani ya Xiaomi nao wamesema wapo njiani kufanya hivyo.
Simu zenye uwezo wa kukunjwa na kukunjuliwa na kuongeza eneo la display zinaonekana zitaweza kusaidia kufanya simu zizidi kuwa na uwezo wa kubadilika muonekano kutokana na mahitaji husika ya mtumiaji kwa wakati fulani.
Mfano wakati wa kupiga na kupokea simu unaweza ukawa unatumia simu ikiwa na display ndogo ila pale unapotaka kutazama video YouTube au kwa Netflix ukakunjua na hivyo kuongeza eneo la display ili kuona video kwa uzuri zaidi.
Rais wa kampuni ya Xiaomi, Bwana Lin Bin ameonesha simu yao ambayo wanategemea itaenda kwa jina la Xiaomi MIX Flex au Xiaomi Dual Flex, na wana lengo la kuwa wa kwanza kabisa kuingiza simu yenye display ya mkunjo sokoni.
Simu hii ikiwa imefunguliwa ina kuwa na display ya ukubwa wa inchi 6 wakati ikikunjwa inapungua hadi ukubwa wa inchi 3.
Hakuna data kubwa za sifa ya simu hiyo ambazo zimewekwa wazi tayari. Ila watafiti wengi wanategemea simu hiyo kuja na prosesa ya kisasa ya Snapdragon 855 na RAM ya GB 8, bei bado ila kwa kampuni ya Xiaomi inategemewa kuja na bei nafuu sana ukilinganisha na Samsung.
Kampuni ya Xiaomi wanategemewa kushiriki katika maonyesho ya kiteknolojia ya Mobile World Congress (MWC) 2019, tarehe 24 Februari, na wengi wanategemea kuna uwezekano mkubwa simu hiyo ikaoneshwa kwa undani kwenye maonyesho hayo.