Baada ya utafiti wa muda mrefu matokeo ya majaribio ya wanasayansi nchini Italia yanaonesha kuna uwezekano mkubwa wa kuwa na chanjo ya UKIMWI (Upungufu wa Kinga Mwilini) katika miaka ya hivi karibuni.
Utafiti wao mpaka ulipofikia imethibitika kwamba chanjo waliyoitengeneza imetoa majibu ambayo waliyakusudia, yaani kuwa na uwezo wa kutoa kinga dhidi ya VVU (Virusi vya Ukimwi) na pia kuwa na uwezo wa kutengeneza kinga ya mwili ya kuharibu VVU kwa wale ambao tayari wana maambukizi.
Utaratibu wa sasa kwa wanaoishi na VVU ni kutumia dawa za ARV kila siku kwa siku zote za uhai wao. Dawa za ARV zimeboreshwa sana na kufanya mtu anayeishi VVU kuweza kuwa na afya bora kwa kuimarisha kinga ya mwili na kupunguza uwezo wa VVU kushinda kinga za mwili – hivyo kuepusha kuwa katika hali ya magonjwa nyemelezi – yaani UKIMWI.
Matokeo ya utafiti yanaonesha chanjo hiyo ina uwezo wa kupunguza zaidi ya asilimia 90 ya utengenezaji wa Virusi vya Ukimwi -. kwa kuzuia na kuharibu eneo kuu la utengenezaji wa virusi (virus reservoir).
Chanjo hiyo ambayo bado ipo kwenye majaribio inailenga aina maalum ya “protini ijulikanayo kama HIV-1 Tat. Protein hii ni muhimu katika maisha ya virusi vinavyosababisha ugonjwa wa Ukimwi.
Kwa sasa utafiti huu umehusisha majaribio ya nyani na wakifikia hatua ya kuhakikisha ni salama zaidi majaribio kufanyika kwa binadamu basi itakuwa ni hatua kubwa.
Sifa nyingine kuu ya ugunduzi wao ni kwamba sindano ya chanjo hii itafanyika mara moja tuu, iwe kabla ya mtu kapata maambukizi au hata baada ya kupata maambukizi. Kwa ambao hawajapata maambukizi bado chanjo itasaidia kuzuia virusi hivyo kuweza kuingia kwenye mfumo wa mwili na kwa wale ambao tayari wana maambukizi chanjo itahakikisha ina pambana na eneo kuu la mazalio ya virusi hivyo.
Matokeo ya utafiti huu yamechapishwa katika jarida la Frontier in Immunology.
Vipi mtazamo wako juu ya maendeleo makubwa hivi?
Vyanzo: ANSA, HIVPlusMag na vingine