Kampuni ya simu ya Vodacom kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) zimepewa siku 30 kutoa suluhisho la wizi wa mtandao kwa wateja wake.
Agizo hilo limetolewa Julai 23 na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Mhandisi Isaack Kamwelwe wakati alipotembelea ofisi za TCRA ikiwa ni mara ya kwanza tangu alipohamishiwa wizara hiyo Julai mosi katika mabadiliko ya Baraza la Mawaziri yaliyofanywa na Rais John Magufuli.
Mhe. Kamwelwe alisema kabla hawajaweka sheria itakayowalazimu kurudisha fedha za mteja itakayoibwa, lazima wakae kuangalia watu hao kama ni wafanyakazi waliofukuzwa.
Takwimu za matukio ya wizi wa mtandao zilizotolewa na Jeshi la Polisi nchini, zinathibitisha kuwa kuanzia Oktoba 2016 hadi Machi 2017 mambo yalikuwa kama ifuatavyo:-
Mkoa wa Dar Es Salaam ulikuwa na matukio 1,423 ya wizi wa fedha kwa njia ya mtandao wa simu huku ukifuatiwa kwa mbali na mkoa wa Mwanza ambao ulikuwa na matukio 659.
Kampuni zilizohusika na miamala hiyo ni Vodacom (M-Pesa), Tigo (Tigo Pesa), Airtel (Airtel Money), Zantel (Easy Pesa) na Halotel (Halopesa).