Viongozi wa makundi ya whatsApp (Group Admins) karibuni watapewa uwezo mkubwa wa kudhibiti wanachama wa makundi yao kuweza kuzuia au kufuta ujumbe utakaotumwa katika makundi yao.
WhatsApp imekusudia kuleta maboresho ya kipengele hicho baada ya maombi ya watumiaji wengi kuomba kuwe na kipengele cha namna hiyo kwa muda mrefu.
Maboresho hayo yanatarajiwa kuwepo kwa watumiaji wote wa WhatsApp katika siku za usoni na tayari kwa watumiaji wa toleo la whatsApp beta kwenye baadhi ya nchi wameanza kupata kipengele hicho kwa majaribio.
Ni kwamba maboresho hayo yatamuwezesha kiongozi wa kundi la WhatsApp kuzuia ujumbe wa mwanachama kuonekana katika kundi mpaka atakapoidhinisha uonekane katika kundi zima au anaweza kuruhusu ujumbe uonekane na kama ataona kuna haja ya kuufuta basi anaweza kufanya hivyo.
Kwa mujibu wa tovuti ya WABetaInfo ambayo imekuwa ikifuatilia kwa karibu kila kipengele kipya kutoka WhatsApp ni kwamba kiongozi wa kundi anaweza kuzuia au kufuta Picha za mnato, Video, Documents, GIF, Ujumbe wa Sauti na ujumbe wa maneno.
Vilevile kiongozi wa kundi anaweza kuruhusu yeyote kutuma lakini akaweza kufuta kama ataona kilichotumwa kipo kinyume na taratibu za kundi. Kipengele hicho kinafafana na kile kilichopo katika makundi ya Facebook ambapo kiongozi wa kundi anaweza kuzuia ujumbe kutoonekana kwa wanakundi wengine mpaka aidhinishe yeye au kufuta kilichotumwa.
Ni kama kwenye Telegram….
Katika app ya Telegram ambapo wanakundi hawawezi kutuma ujumbe wowote isipokuwa kiongozi wa kundi husika.
Aidha, kipengele kingine kinachotarajiwa kuongezwa ni uwezo wa kusahihisha jina la kundi au Icon yake (utambulisho wa picha ya kundi) kwa wanachama pekee tu ambao kiongozi wa kundi atawaidhinisha na si yeyote kwenye kundi ataweza kufanya hivyo kama ilivyo sasa kitu ambacho kimekuwa kikileta usumbufu.