Ukiritimba kwenye soko la App Store. Mahakama ya juu Marekani (Supreme Court) imetoa ruhusa kwa kundi la watumiaji wa iPhone kufungua kesi dhidi ya Apple na ukiritimba (monopoly) waliouweka kwenye eneo la upakuaji apps.
Maombi ya kesi hiyo yalifunguliwa tokea mwaka 2011 na sasa baada ya majaji kadhaa kukaa na kupitia wameona kuna kesi ya kusikilizwa.
Watumiaji hao wanadai haki ya uwepo wa masoko mengine ya apps katika vifaa vya Apple ili kuleta ushindani, kwa sasa wanaamini bei wanazolipa kwa ajili ya kupata apps ndani ya soko hilo zimewekwa juu ili kufaidisha kampuni ya Apple na kwa kuwa hakuna namna nyingine ya kupata apps basi watumiaji wanaendelea kunyonywa.
Data kutoka tovuti ya data na utafiti ya Statista inasema watumiaji wa Marekani wametumia zaidi ya dola bilioni 46.6 za Marekani katika huduma za ununuaji apps, na ulipiaji mwingine wa apps kwa mwaka 2018 (Kumbuka Dola 1 ni takribani Tsh 2,200 – 2,300).
Wengi wanataka watumiaji wa iPhone wawe na uwezo wa kuweka apps moja kwa moja kutoka kwa mtengenezaji app au kupitia masoko mengine ya apps tofauti na mfumo wa sasa ambao mtu hawezi kupata app bila kutumia app ya AppStore ya Apple.
Watumiaji wa Android wana uhuru mkubwa katika eneo hili ambapo wanauwezo wa kupakua apps tofauti za masoko ya apps nje ya Google Playstore. Pia wanaweza kwenda moja kwa moja kwenye tovuti za watengenezaji apps husika na kupakua app wanayotaka.
Kama kesi hii itakuja kuamuliwa upande wa watumiaji – yaani Apple kutakiwa kuweka uhuru, itakuwa ni pigo kubwa kwa Apple. Tayari Apple wameshaona mauzo ya simu zao yakishuka ukilinganisha na zamani, na tayari soko lao la apps limekuwa moja ya sehemu muhimu ya kuwaingizia mapato kwa watumiaji wa simu mpya na zamani.
Endelea kutembelea Teknokona tutakujuza maendeleo ya kesi hii.
Chanzo: BBC