Unataka simu ila bado unajiuliza uchague au usichague simu za iPhone au uchukue za Android? Katika makala hii tunakuelezea mambo muhimu ya kufahamu kuhusu simu za iPhone ili kukusaidia pale unapofanya maamuzi ya kununua.
Kumbuka mara nyingi tunaponunua simu huwa tunalenga kukaa nayo kwa muda mrefu kiasi na ata kama ni muda mfupi basi unataka kuwa na uhakika yale unayoyapenda utaweza kuyafanya kwenye simu husika.
Faida za kununua na kutumia simu za iPhone:
>Programu endeshaji inayofanya kazi kwa ufanisi.
Kama kuna sehemu ambayo Apple wamewashinda Google katika eneo la simu basi ni jinsi ambavyo wanasimamia programu endeshaji ya iOS kuhakikisha inafanya kazi kwa ufanisi mkubwa ukilinganisha na hali inayojitokeza kwa Android. Una uhakika wa kutumia simu yako kwa ufanisi mzuri tuu kwa miaka kadhaa tokea uinunue.
>Kupata masasisho mapya (Updates)
Makampuni ya utengenezaji simu yanayotumia Android huwa yanachukua toleo zuri lisilo na makorokocho mengi kutoka Google na kisha kila kampuni huingiza apps na kufanya maboresho mengine kwa Android kiasi cha kuathiri ufanisi na ubora wake. Na hili ndilo linalosababisha Google kushindwa kutuma masasisho (updates) za moja kwa moja kwenda kwenye simu za Android wakati ukinunua simu ya iPhone unakuwa una uhakika wa kupata matoleo mapya ya iOS kwa haraka na ufanisi wa hali ya juu.
>Muonekano rahisi kwa utumiaji
Kwa watu ambao si watundu sana na wanapenda simu janja (smartphone) huku utumiaji wao mkuu ukiwa ni kupiga na kupokea simu, kupiga picha na kutumia ujumbe mfupi basi iPhone zina muonekano rafiki zaidi kwao. Ni rahisi kuitumia haraka kwa maeneo hayo, haiitaji ujuzi na utundu sana.
>Apps
Ni rahisi zaidi kuwa na uhakika wa apps salama na zenye kufuata sheria kali ya kiwango cha ubora katika soko la apps la Appstore. Soko la apps la Google limejikuta mara kwa mara katika matatizo ya kuruhusu apps zenye ubora wa hali ya chini na ata kuathiri utendaji kazi wa simu zinapotumika.
>Ubora wa Kamera na simu zenyewe
Apple wanajitahidi sana kuhakikisha simu zao zinakuja na kiwango cha ubora wa juu katika eneo la kamera na ata simu zenyewe kwa ujumla wake. Ni makampuni machache yanayotengeneza simu zinazotumia Android yanayojitahidi kufikia na kuvipita viwango vya ubora huo.
Hizo ni faida kadhaa, lakini je kuna mapungufu gani katika utumiaji wa iPhone?
>Utumiaji wa mafaili kutoka mtandaoni
Wakati kama wewe ni mtumiaji wa simu za Android unaweza kushusha mafaili mbalimbali kutoka mtandaoni kama vile nyimbo za muziki n.k utaweza kuyatumia mafaili hayo moja kwa moja – hali ni tofauti kwa watumiaji wa iPhone. Kule utaweza kushusha picha na baadhi ya mafaili tu kama pdf na kuweza kutumia.
>Chaja
Wakati karibia zaidi ya asilimia 80 ya simu janja za Android zinaweza kutumia chaja ya aina moja hali ni tofauti kwa watumiaji wa iPhone. Hii ina maanisha kama umesahau chaja sehemu basi kuna nafasi kubwa ukashindwa kuchaji kifaa chako sehemu unayoenda – kwani ukweli ni kwamba bado watumiaji wa simu za Android ni wengi zaidi na wanaweza kutumia chaja ile ile.
>Ugumu wa kubadili muonekano
Hii ni sehemu nyingine ambayo simu za Android zinafanya vizuri zaidi. Kwa simu za Android una uhuru mkubwa wa kufanya mabadiliko ya kimuonekano (themes). Kwenye iPhone badiliko kubwa unaloweza kufanya ni la wallpaper tuu. Wakati kwa Android unaweza badilisha mambo mengi zaidi – icons, rangi ya menu, n.k.
>Unataka ujazo mkubwa? Nunua simu yenye ujazo mkubwa kwa bei ya juu zaidi
Hii ni sehemu nyingine ambapo Apple wanahakikisha wanapata pesa nyingi zaidi kutoka kwa wanunuaji wa iPhone. Wakati kwa simu nyingi za Android unaweza kununua simu ya ujazo mdogo na ukanunua memori kadi (SD Card) ya bei rahisi na hivyo kuongeza ujazo wa simu yako. Kwa iPhone hakuna eneo la kutumia memori kadi na hivyo ukitaka ujazo zaidi itakubidi ununua simu ya toleo la ujazo wa juu ambalo nalo linauzwa kwa bei ya juu zaidi.
>Ata kuweka kitu kidogo tuu unaitaji kompyuta yenye programu ya iTunes
Wakati watumiaji wa Android wanaweza kudownload nyimbo na kuweza kuzitumia moja kwa moja kwenye simu zao – pia ata kuchomeka kwenye kompyuta na kuweka nyimbo na kitu kingine chochote moja kwa moja bila uitaji wa programu spesheli, hali ni tofauti kwa watumiaji wa iPhone. Kuweka vitu kama nyimbo n.k kwenye simu za iPhone zitakuitaji kutumia kompyuta, tena yenye programu spesheli ya iTunes.