Zikiwa zimebaki siku chache kufanyika tukio la uzinduzi wa Simu Janja mpya za Kampuni ya Apple kuna mambo machache yatakuwa tofauti kama ilivyo kwa miaka mingine iliyopita.
Moja ya jambo kubwa ni sehemu ya uzinduzi wa tukio hilo. Kwa mara ya kwanza litakuwa linafanyika katika ukumbi mpya kabisa unaojulikana kama Steve Jobs Theatre.
Eneo panapofanyikia uzinduzi huo ndipo patakapo kuwa makao makuu ya Apple. Na ndani ya jengo hilo ndipo ulipo ukumbi wa Steve jobs Theatre. Makao makuu hayo yapo Cupertino, California, Marekani.
Ujenzi huo unaokaribia kukamilika, inaelezwa gharama za pesa za ujenzi wa eneo hilo zinakadiriwa kufika Dola Bilioni 5.
Makao makuu hayo yatakayojulikana kama Apple park au maarufu kwa ‘Spaceship’ yamejengwa kwa muonekano kama wa uwanja wa Mpira ambapo ofisi nyingi zitakuwa zinazunguka eneo lote la Apple Park.
Mzunguko wa Jengo hilo kutakuwa na ofisi nyingi, ikiwemo migahawa, sehemu za michezo, nyumba za wafanyakazi zipatazo 12,000. na kutazungukwa na miti ipatayo 9,000 ikiwemo ya matunda ya Tufaa (Apple), misherisheri na mingine mingi.
kutakuwa na vituo vya utafiti na barabara kwa ajili ya magari na baiskeli ambazo zitakuwepo kurahisisha kwa wafanyakazi kutoka eneo moja kwenda lingine.
Wazo la ujenzi huo wa Apple Park lilianza kwa muanzilishi msaidizi na mkurugenzi Mkuu wake marehemu Steve Jobs aliyefariki mwaka 2011 kwa ugonjwa wa Saratani ya kongosho.