Ingawa soko la simu janja katika mwaka 2018 limeshuka duniani kote ni soko la simu janja Afrika ndilo linaendelea kuonesha ukuaji mzuri wa wastani wa mwaka hadi mwaka.
Data za IDC (International Data Corporation) za Machi mwaka huu zinaonesha soko la simu janja barani Afrika lilikua kwa asilimia 2.3 ndani ya mwaka 2018 hadi kufikia mauzo ya simu janja milioni 88.2 – masoko ya Naijeria, Afrika Kusini na Misri yakiongoza.
Katika eneo la makampuni yanayoongeza barani Afrika hii ni pamoja na kampuni ya Transsion inayomiliki simu za Tecno, Infinix na Itel. Samsung na Huawei wakifuata.
Mauzo ya simu janja kwa mwaka 2018 barani Afrika
Katika robo tatu ya mwaka 2019 kumekuwa na ukuaji upande wa Samsung
- Transsion: Asilimia 33.1
- Samsung: Asilimia 24.5
- Huawei: 11.8%
Ingawa Transsion inayomiliki Tecno, Infinix na Itel iliongeza kwa idadi ya mauzo ni Samsung ndio aliyeongoza kwa thamani ya mauzo (yaani kimapato kutoka simu janja alizouza – kulingana na bei zake n.k).
Kwa thamani ya mauzo kwa mwaka 2018 Samsung alichukua asilimia 36.9, Transsion ikichukua asilimia 20.2 na huku Huawei ikichukua asilimia 12.4.
Bado soko la simu ambazo sio simu janja (featured phones) lipo juu, hii ikiwa ni asilimia 54 ya simu zote zinazouzwa.
Kimauzo makampuni haya matatu yanawakilisha asilimia 69.5 ya simu janja zote zilizoingia sokoni kwa mwaka 2018. Asilimia nyingine ikichukuliwa na makampuni ya ndani ya bara la Afrika na makampuni mengine ya nje hii ikiwa ni pamoja na Apple, Xiaomi na mengineyo.