Toleo jipya la programu endeshaji la Android maarufu kama Oreo limepata takwimu za kustaajabisha hasa baada ya toleo hilo kupewa sifa lukuki lakini imekuwa tofauti kwa maana ya watumiaji wa simu janja wamefanya masasisho na kuhamia kwenye toleo la Oreo.
Kwa takwimu zilizotoka hivi karibuni zinaonyesha bado watu hawana mwamko wa kutaka kutumia toleo la Android 8.0 kwenye vifaa vyao (simu janja). Takwimu zinaonyesha kuwa ni 0.3% tu ya simu janja ndio zenye kutumia/zimefanya masasisho kutoka toleo moja hadi Oreo.
Sababu kubwa ambayo imeonekana kusababisha Android 8.0 kutumika kwenye simu janja chache ni kwamba toleo hilo linakubali kwenye simu janja za Nexus na Pixel tu kitu ambacho watumiaji wengi wa Android hawana simu hizo.
Je, ni matoleo gani ya Android OS yanayotumika kwa wingi mpaka sasa?
Matoleo ya kabla ya Oreo yaani Androd 7.0 na 7.1 yanaonekana kuendelea kupendwa na kutumika kwenye simu janja kwa 17.6% (kwa Android 7.1) na 3% (kwa Android 7.0) ya simu janja zote zinazotumia Android; zaidi ya simu janja bilioni 2 zikitumia matoleo hayo mawili.
Kwa mwezi Novemba Android Marshmallow v6.0 inatumika zaidi kwa 30.9% ya simu janja/tabiti na ndio kinara kwa maana ya kwamba bado inatumika kwa asilimia kubwa, hasa kwenye tabiti. Kwa mwezi uliopita ilikuwa ikitumika kwa 32%.
Lollipop v5.0 na v5.1 zinatumika kwenye simu janja/tabiti kwa 6.4% na 20.8% mtawaliwa kwa simu janja/tabiti zote zinazotumia Android. Kwa mwezi uliopita zote kwa pamoja zilikuwa zikitumika 27.7%.
Matoleo mengine kama Android Jelly Bean v4.1.x, v4.2.x na v4.3 yanatumika kwa 2.2%, 3.1% na 0.9% mtawaliwa. KitKat inatumika kwa 13.8% ya vifaa vyote vyenye Android huku Android Gingerbread na Ice Cream zikitumika kwa 0.5% ya vifaa vya Android.
Wewe msomaji wetu toleo gani la Android limekuvutia sana na huoni haja ya kufanyia masasisho simu janja/tabiti yako na kuhamia kwenye toleo la Android 8.0 (Oreo)? Tupe maoni yako na usiache kutufuatilia kila siku.
Gadgets Now, Gadgets 360