Je tokea uupdate kwenda toleo jipya la Februari Windows 10 kwenye kompyuta yako imekuwa inasumbua sumbua? Fahamu sasisho hilo la Windows 10 lina matatizo.
Microsoft wamesema sasisho jipya la Windows 10 lililotolewa Februari – toleo 1809 KB4482887 linaleta matatizo kadhaa kwa baadhi ya kompyuta duniani kote.
Kama umesasisha kompyuta yako katika kipindi hicho na unaona kuna vitu kama vile kipanya (mouse) haifanyi kazi vizuri, au pale unapocheza magemu kwenye kompyuta yako inakuwa katika hali ya kugoma goma/kuganda basi fahamu sasisho hili ndio limesababisha.
Kwa kiasi kikubwa kundi la watu wanaotumia kompyuta zao za Windows kwa ajili ya kucheza magemu ndio wameathirika zaidi na wengi wamekasirishwa sana na ucheleweshaji wa taarifa hii. Kwani kuna waliokuwa wamechukua hatua mbalimbali kujaribu kurekebisha matatizo waliyokuwa wakiyapata, wengi wakifikiri ni tatizo la kiufundi la kompyuta zao.
Microsoft wameshauri watu wenye toleo hili kuliondoa mara moja (uninstall), na pia tayari wanafanyia kazi kuleta sasisho jipya la kuondoa tatizo hilo.
Chanzo: Windows Latest n.k