Kwa mujibu wa taarifa za kuaminika imeelezwa kuwa Samsung wanataka kuleta simu janja mpya ikiwa ni muendelezo wa kutoa simu ambazo zinatoka kwenye familia moja, Samsung S8 Lite ipo njiani kutambulishwa.
Ni mwaka jana tu, 2017 Samsung walileta simu janja za S8 na S8 plus sasa ni wakati wa bidhaa nyingine kuja ili kuongeza kasi ya ushindani na kuwafurahisha wapenzi wa simu janja za Samsung. Unajua Samsung Galaxy S8 Lite itakuwa na sifa gani? Fuatilia pamoja nasi:
Prosesa/Ukubwa (ubora) wa kioo.
Hapa unaweza ukashangaa lakini ndio ukweli wenyewe, simu ya Samsung Galaxy S8 Lite itakuwa na prosesa ya Snapdragon 660 wakati S8/S8+ zina Snapdragon 835. Ukubwa wa kioo ni sawa tu mtangulizi wake, ina inchi 5.8 lakini pia ubora wa muonekano wa vitu kwenye kioo ni 2220x1080p huku kwenye S8 zote mbili ubora picha ni 2960x1440p.
Diski uhifadhi/RAM.
Simu ya Samsung Galaxy S8 Lite inakuja na diski uhifadhi wa GB 64 pamoja na RAM ya GB 4. Kwa kiwango hicho cha RAM pamoja na ukubwa wa nafasi ya kutunza vitu kwenye simu suala zima la simu kukwamakwama wkati inapofanya kazi itakuwa ngumu kidogo ila si kwamba halitowezekana.
Betri/Rangi.
Samsung S8 Lite itakuwa na betri yenye 3000mAh na kama kawaida ya simu nyingi betri lake halitoki. Kwa taarifa zilizovuja zinaeleza kuwa simu hii (S8 Lite) itakuwa katika rangi mbili; Nyeusi na Nyekundu isiyokolea.
Kamera/Programu endeshi.
Inategemewa kuwa Samsung Galaxy S8Lite intakuwa na kamera moja nyuma nyenye MP 16 na ile ya mbele itakuwa na MP 8. Kuhusu programu endeshi, S8 Lite inaaminika kuwa itakuja na toleo la Android 8 maarufu kama Oreo.
Hizo ndio sifa zake kwa uchache huku ikitegemewa kuzinduliwa Mei 21 huko nchini Uchina. Na kiujumla sifa za S8 Lite ndio maana halisi ya neno “Lite“; ni lazima isiwe bora sana kuzidi yule aliyetangulia.
Vyanzo: Tech Spot, Gadgets 360.
One Comment
Comments are closed.