Samsung wanaonekana kupendezwa na mtindo wa kutoa simu janja kutoka familia moja kwa mkupuo lakini zikitoka matoleo tofauti tofauti kama vile walivyotoa Samsung Galaxy S10 nne (4) miezi kadhaa iliyopita, sasa kitu hicho kinatazamiwa kujirudia watakapotoa Samsung Galaxy Note 10.
Wakati ulimwengu ukitaka kuondokana na fununu za kila mara kuhusu Samsung Galaxy Note 10 inaonekana bado haijatosha kutoa sifa za simu husika na kwa mujibu wa ripoti ya hivi karibuni rununu hiyo itakuja katika matoleo manne tofauti; simu mbili zina na teknolojia ya 5G huku mbili nyingine ni za 4G. Ripoti hiyo haikuishia hapo bali imekwenda mbali zaidi na kutoa sifa za ndani kidogo kuhusu bidhaa hizo kutoka Samsung:
Urefu wa kioo
Inaelezwa kuwa simu mbili kati ya nne zitakuwa na kioo cha urefu wa inchi 6.75 huku zile mbili nyingine zitakuwa na inchi 6.28.
Kamera
Upande wa kamera pia simu hizo zitakuwa na utofauti kwani rununu mbili kati ya nne zitakuwa na kamera nne huku zile mbili nyingine zitakuwa na kamera tatu (3). Kwa mantiki hiyo ni wazi kwamba zile ambazo zitakuwa na vipengele bora zaidi kuliko wenzake ndio zitakuwa kama kiongozi wa simu kwenye familia hiyo
Majina ya simu hizo bado hayajafahamika mbali na kwamba zote zitakuwa ni Samsung Galaxy Note 10. Saa inatupasa kusubiri ili kuweza kujua undani kamili wa simu hizo zinazotarajiwa kutoka miezi michache ijayo.
Vyanzo: GSMArena, Tech The Lead