Kwa takribani wiki kadhaa zilizopita kulikuwa na tetesi za kuzinduliwa kwa simu hiyo na kwa mujibu wa taarifa rasmi ni kwamba Nubia Red Magic 3 itazinduliwa tarehe 28 Aprili 2019 huko Beijing-Uchina.
Meneja mkuu wa Kampuni hiyo Ni Fei ametangaza mapema wiki hii kupitia mtandao wa Weibo kwamba tukio la uzinduzi wa Nubia Red Magic 3 uitafanyika katika kituo cha RNG eSports Center huko Beijing.
Baadhi ya sifa za simu hiyo zimewekwa wazi ikiwemo ukubwa Betri ndani ya simu hiyo. Imeelezwa simu hiyo itakuwa na Betri yenye ujazo wa 5000mAh pamoja na Prosesa ya Snapdragon 855 na RAM itakuwa na 12GB. Rununu ambazo tayari zimeshaingia sokoni kutoka kwa kampuni husika ni Nubia Red Magic Mars, Nubia X, Nubia Z18, Nubia Red Magic 2, Nubia V18, Nubia N3, Nubia Z17s.
Nubia ni kampuni ya Uchina inayojihusisha na uzalishaji wa simu za kisasa iliyoanzishwa miaka 4 (2015) iliyopita ikiwa na makao makuu yake mji wa Shenzhen, Guangdong. ZTE ikiwa na sehemu ya hisa katika kampuni hiyo, simu zake zimekuwa zikiuzwa Ulaya, Amerika Kusini, Kusini Mashariki ya Asia, Asia ya Kusini, Mashariki ya Kati na baadhi ya nchi za Afrika.